Zaburi 18:1-50 ONEN
[1] Nakupenda wewe, Ee BWANA, nguvu yangu. [2] BWANA ni mwamba wangu, ngome yangu na mwokozi wangu, Mungu wangu ni mwamba, ambaye kwake ninakimbilia. Yeye ni ngao yangu na pembe ya wokovu wangu, ngome yangu. [3] Ninamwita BWANA anayestahili kusifiwa, nami ninaokolewa kutoka kwa adui zangu. [4] Kamba za mauti zilinizunguka, mafuriko ya maangamizi yalinilemea. [5] Kamba za kuzimu zilinizunguka, mitego ya mauti ilinikabili. [6] Katika shida yangu nalimwita BWANA, nilimlilia Mungu wangu anisaidie. Kutoka hekaluni mwake alisikia sauti yangu, kilio changu kikafika mbele zake, masikioni mwake. [7] Dunia ilitetemeka na kutikisika, misingi ya milima ikatikisika, vilitetemeka kwa sababu alikuwa amekasirika. [8] Moshi ukapanda kutoka puani mwake, moto uteketezao ukatoka kinywani mwake, makaa ya moto yawakayo yakatoka ndani mwake. [9] Akazipasua mbingu akashuka chini, mawingu meusi yalikuwa chini ya miguu yake. [10] Alipanda juu ya kerubi akaruka, akapaa juu kwa mbawa za upepo. [11] Alifanya giza kuwa kitu chake cha kujifunika, hema lake kumzunguka, mawingu meusi ya mvua ya angani. [12] Kutokana na mwanga wa uwepo wake mawingu yalisogea, ikanyesha mvua ya mawe na umeme wa radi. [13] BWANA alinguruma kutoka mbinguni, sauti ya Aliye Juu Sana ilisikika. [14] Aliipiga mishale yake na kutawanya adui, naam, umeme mwingi wa radi na kuwafukuza. [15] Mabonde ya bahari yalifunuliwa, na misingi ya dunia ikawa wazi kwa kukaripia kwako, Ee BWANA, kwa uvumi wa pumzi kutoka puani mwako. [16] Alinyoosha mkono kutoka juu na kunishika; alinitoa kutoka kilindi cha maji makuu. [17] Aliniokoa kutoka adui wangu mwenye nguvu nyingi, kutoka adui zangu waliokuwa na nguvu nyingi kuliko mimi. [18] Walinikabili siku ya msiba wangu, lakini BWANA alikuwa msaada wangu. [19] Alinileta nje mahali penye nafasi tele, akaniokoa kwa kuwa alipendezwa nami. [20] BWANA alinitendea sawasawa na uadilifu wangu; sawasawa na usafi wa mikono yangu amenilipa. [21] Kwa maana nimezishika njia za BWANA; sijatenda ubaya nikamwacha Mungu wangu. [22] Sheria zake zote zi mbele yangu, wala sijayaacha maagizo yake. [23] Nimekuwa sina hatia mbele zake, nami nimejilinda nisitende dhambi. [24] BWANA amenilipa sawasawa na uadilifu wangu; sawasawa na usafi wa mikono yangu machoni pake. [25] Kwa yeye aliye mwaminifu, unajionyesha kuwa mwaminifu, kwa asiye na hatia, unajionyesha kutokuwa na hatia. [26] Kwa aliye mtakatifu, unajionyesha kuwa mtakatifu, lakini kwa aliyepotoka, unajionyesha kuwa mkaidi. [27] Wewe huwaokoa wanyenyekevu, lakini huwashusha wenye kiburi. [28] Wewe, Ee BWANA, unaifanya taa yangu iendelee kuwaka; Mungu wangu hulifanya giza langu kuwa mwanga. [29] Kwa msaada wako naweza kushinda jeshi, nikiwa pamoja na Mungu wangu nitaweza kuruka ukuta. [30] Kuhusu Mungu, njia yake ni kamilifu, neno la BWANA halina dosari. Yeye ni ngao kwa wote wanaokimbilia kwake. [31] Kwa maana ni nani aliye Mungu zaidi ya BWANA? Ni nani aliye Mwamba isipokuwa Mungu wetu? [32] Mungu ndiye anivikaye nguvu na kufanya njia yangu kuwa kamilifu. [33] Huifanya miguu yangu kama miguu ya kulungu, huniwezesha kusimama mahali palipo juu. [34] Huifundisha mikono yangu kupigana vita; mikono yangu inaweza kupinda upinde wa shaba. [35] Hunipa ngao yako ya ushindi, nao mkono wako wa kuume hunitegemeza, unajishusha chini ili kuniinua. [36] Huyapanua mapito yangu, ili miguu yangu isiteleze. [37] Niliwafuatia adui zangu na nikawapata, sikurudi nyuma mpaka walipoangamizwa. [38] Niliwaseta hata hawakuweza kuinuka tena; walianguka chini ya miguu yangu. [39] Ulinivika nguvu kwa ajili ya kupigana vita; uliwafanya adui zangu wasujudu miguuni pangu. [40] Uliwafanya adui zangu wageuke na kukimbia, nami nikawaangamiza adui zangu. [41] Walipiga yowe, lakini hapakuwepo na yeyote wa kuwaokoa; walimlilia BWANA, lakini hakuwajibu. [42] Niliwaponda kama mavumbi yanayopeperushwa na upepo; niliwamwaga nje kama tope barabarani. [43] Umeniokoa kutokana na mashambulizi ya watu; umenifanya kuwa kiongozi wa mataifa, watu ambao sikuwajua wananitumikia. [44] Mara wanisikiapo hunitii, wageni hunyenyekea mbele yangu. [45] Wote wanalegea, wanatoka katika ngome zao wakitetemeka. [46] BWANA yu hai! Sifa ni kwa Mwamba wangu! Atukuzwe Mungu Mwokozi wangu! [47] Yeye ndiye Mungu anilipiziaye kisasi, awatiishaye mataifa chini yangu, [48] aniokoaye na adui zangu. Uliniinua juu ya adui zangu; uliniokoa toka kwa watu wajeuri. [49] Kwa hiyo nitakusifu katikati ya mataifa, Ee BWANA; nitaliimbia sifa jina lako. [50] Humpa mfalme wake ushindi mkuu, huonyesha fadhili zake kwa mpakwa mafuta wake, kwa Daudi na wazao wake milele.
