[1] Msifuni BWANA. Tazama jinsi ilivyo vyema kumwimbia Mungu wetu sifa, jinsi inavyopendeza na kustahili kumsifu yeye! [2] BWANA hujenga Yerusalemu, huwakusanya Israeli walio uhamishoni. [3] Anawaponya waliovunjika mioyo na kuvifunga vidonda vyao. [4] Huzihesabu nyota na huipa kila moja jina lake. [5] Bwana wetu ni mkuu na mwenye uwezo mwingi, ufahamu wake hauna kikomo. [6] BWANA huwahifadhi wanyenyekevu lakini huwashusha waovu mpaka mavumbini. [7] Mwimbieni BWANA kwa shukrani, mpigieni Mungu wetu kinubi. [8] Yeye huzifunika anga kwa mawingu, huinyeshea ardhi mvua, na kuzifanya nyasi kuota juu ya vilima. [9] Huwapa chakula mifugo na pia makinda ya kunguru yanapolia. [10] Furaha yake haipo katika nguvu za farasi, wala furaha yake kwenye miguu ya mwanadamu. [11] BWANA hupendezwa na wale wamchao, wale wanaoweka tumaini lao katika upendo wake usiokoma. [12] Mtukuze BWANA, ee Yerusalemu, msifu Mungu wako, ee Sayuni, [13] kwa maana huimarisha makomeo ya malango yako na huwabariki watu wako walio ndani yako. [14] Huwapa amani mipakani mwenu na kukushibisha kwa ngano safi kabisa. [15] Hutuma amri yake duniani, neno lake hukimbia kasi. [16] Anatandaza theluji kama sufu na kutawanya umande kama majivu. [17] Huvurumisha mvua yake ya mawe kama changarawe. Ni nani awezaye kustahimili ukali wa baridi yake? [18] Hutuma neno lake na kuviyeyusha, huvumisha upepo wake, nayo maji hutiririka. [19] Amemfunulia Yakobo neno lake, sheria zake na maagizo yake kwa Israeli. [20] Hajafanya hivyo kwa taifa lingine lolote, hawazijui sheria zake. Msifuni BWANA.