[1] Msifuni BWANA. Msifuni BWANA kutoka mbinguni, msifuni juu vileleni. [2] Msifuni, enyi malaika wake wote, msifuni yeye, enyi jeshi lake lote la mbinguni. [3] Msifuni yeye, enyi jua na mwezi, msifuni yeye, enyi nyota zote zingʼaazo. [4] Msifuni yeye, enyi mbingu zilizo juu sana, na ninyi maji juu ya anga. [5] Vilisifu jina la BWANA kwa maana aliamuru navyo vikaumbwa. [6] Aliviweka mahali pake milele na milele, alitoa amri ambayo haibadiliki milele. [7] Mtukuzeni BWANA kutoka duniani, ninyi viumbe vikubwa vya baharini na vilindi vyote vya bahari, [8] umeme wa radi na mvua ya mawe, theluji na mawingu, pepo za dhoruba zinazofanya amri zake, [9] ninyi milima na vilima vyote, miti ya matunda na mierezi yote, [10] wanyama wa mwituni na mifugo yote, viumbe vidogo na ndege warukao, [11] wafalme wa dunia na mataifa yote, ninyi wakuu na watawala wote wa dunia, [12] wanaume vijana na wanawali, wazee na watoto. [13] Wote na walisifu jina la BWANA, kwa maana jina lake pekee limetukuka, utukufu wake uko juu ya nchi na mbingu. [14] Amewainulia watu wake pembe, sifa ya watakatifu wake wote, ya Israeli, watu walio karibu na moyo wake. Msifuni BWANA.