[1] Nitakutukuza wewe, Mungu wangu Mfalme, nitalisifu jina lako milele na milele. [2] Kila siku nitakusifu na kulitukuza jina lako milele na milele. [3] BWANA ni mkuu, anayestahili kusifiwa sana, ukuu wake haupimiki. [4] Kizazi kimoja kitasifia kazi zako kwa kizazi kingine, watasimulia matendo yako makuu. [5] Watasema juu ya utukufu wa fahari ya ukuu wako, nami nitatafakari juu ya kazi zako za ajabu. [6] Watasimulia uwezo wa kazi zako za kutisha, nami nitatangaza matendo yako makuu. [7] Wataadhimisha wema wako mwingi, na wataimba kwa shangwe juu ya haki yako. [8] BWANA ni mwenye neema na mwingi wa huruma, si mwepesi wa hasira, bali ni mwingi wa upendo. [9] BWANA ni mwema kwa wote, ana huruma kwa vyote alivyovifanya. [10] Ee BWANA, vyote ulivyovifanya vitakusifu, watakatifu wako watakutukuza. [11] Watasimulia utukufu wa ufalme wako na kusema juu ya ukuu wako, [12] ili watu wote wajue matendo yako makuu na utukufu wa fahari ya ufalme wako. [13] Ufalme wako ni ufalme wa milele, mamlaka yako hudumu vizazi vyote. BWANA ni mwaminifu kwa ahadi zake zote na mwenye upendo kwa vyote alivyovifanya. [14] BWANA huwategemeza wote waangukao, na huwainua wote waliolemewa na mizigo yao. [15] Macho yao wote yanakutazama wewe, nawe huwapa chakula chao wakati wake. [16] Waufumbua mkono wako, watosheleza haja ya kila kitu kilicho hai. [17] BWANA ni mwenye haki katika njia zake zote, na mwenye upendo kwa vyote alivyovifanya. [18] BWANA yu karibu na wote wamwitao, karibu na wote wamwitao kwa uaminifu. [19] Huwatimizia wamchao matakwa yao, husikia kilio chao na kuwaokoa. [20] BWANA huwalinda wote wampendao, bali waovu wote atawaangamiza. [21] Kinywa changu kitazinena sifa za BWANA. Kila kiumbe na kilisifu jina lake takatifu milele na milele.