[1] Sifa ni kwa BWANA Mwamba wangu, aifundishaye mikono yangu vita, na vidole vyangu kupigana. [2] Yeye ni Mungu wangu wa upendo na boma langu, ngome yangu na mwokozi wangu, ngao yangu ninayemkimbilia, ambaye huwatiisha mataifa chini yangu. [3] Ee BWANA, mwanadamu ni nini hata umjali, Binadamu ni nini hata umfikirie? [4] Mwanadamu ni kama pumzi, siku zake ni kama kivuli kinachopita. [5] Ee BWANA, pasua mbingu zako, ushuke, gusa milima ili itoe moshi. [6] Peleka umeme uwatawanye adui, lenga mishale yako uwashinde. [7] Nyoosha mkono wako kutoka juu, nikomboe na kuniokoa kutoka maji makuu, kutoka mikononi mwa wageni [8] ambao vinywa vyao vimejaa uongo, na mikono yao ya kuume ni midanganyifu. [9] Ee Mungu, nitakuimbia wimbo mpya, kwa zeze yenye nyuzi kumi nitakuimbia, [10] kwa Yule awapaye wafalme ushindi, ambaye humwokoa Daudi, mtumishi wake kutokana na upanga hatari. [11] Nikomboe na uniokoe kutoka mikononi mwa wageni ambao vinywa vyao vimejaa uongo, na mikono yao ya kuume ni midanganyifu. [12] Kisha wana wetu wakati wa ujana wao watakuwa kama mimea iliyotunzwa vizuri, binti zetu watakuwa kama nguzo zilizoviringwa kurembesha jumba la kifalme. [13] Ghala zetu zitajazwa aina zote za mahitaji. Kondoo zetu watazaa kwa maelfu, kwa makumi ya maelfu katika mashamba yetu; [14] maksai wetu watakokota mizigo mizito. Hakutakuwa na kubomoka kuta, hakuna kuchukuliwa mateka, wala kilio cha taabu katika barabara zetu. [15] Heri watu ambao hili ni kweli; heri wale ambao BWANA ni Mungu wao.