[1] Ee BWANA, sikia sala yangu, sikiliza kilio changu unihurumie; katika uaminifu na haki yako njoo unisaidie. [2] Usimhukumu mtumishi wako, kwa kuwa hakuna mtu anayeishi aliye mwenye haki mbele zako. [3] Adui hunifuatilia, hunipondaponda chini; hunifanya niishi gizani kama wale waliokufa zamani. [4] Kwa hiyo roho yangu inazimia ndani yangu, moyo wangu ndani yangu unakata tamaa. [5] Nakumbuka siku za zamani; natafakari juu ya kazi zako zote, naangalia juu ya kazi ambazo mikono yako imezifanya. [6] Nanyoosha mikono yangu kwako, nafsi yangu inakuonea kiu kama ardhi kame. [7] Ee BWANA, unijibu haraka, roho yangu inazimia. Usinifiche uso wako, ama sivyo nitafanana na wale washukao shimoni. [8] Asubuhi uniletee neno la upendo wako usiokoma, kwa kuwa nimeweka tumaini langu kwako. Nionyeshe njia nitakayoiendea, kwa kuwa kwako nainua nafsi yangu. [9] Ee BWANA, uniokoe na adui zangu, kwa kuwa nimejificha kwako. [10] Nifundishe kufanya mapenzi yako, kwa maana wewe ndiwe Mungu wangu, Roho wako mwema na aniongoze katika nchi tambarare. [11] Ee BWANA, kwa ajili ya jina lako, hifadhi maisha yangu, kwa haki yako nitoe katika taabu. [12] Kwa upendo wako usiokoma, nyamazisha adui zangu; waangamize watesi wangu wote, kwa kuwa mimi ni mtumishi wako.