[1] Ee BWANA, niokoe, kutoka kwa watu waovu; nilinde na watu wenye jeuri, [2] ambao hupanga mipango mibaya mioyoni mwao, na kuchochea vita siku zote. [3] Wao hufanya ndimi zao kali kama za nyoka, sumu ya nyoka iko midomoni mwao. [4] Ee BWANA, niepushe na mikono ya waovu; nilinde na watu wenye jeuri wanaopanga kunikwaza miguu yangu. [5] Wenye kiburi wameficha mtego wa kuninasa, wametandaza kamba za wavu wao, wametega mitego kwenye njia yangu. [6] Ee BWANA, ninakuambia, “Wewe ni Mungu wangu.” Ee BWANA, usikie kilio changu na kunihurumia. [7] Ee BWANA Mwenyezi, Mwokozi wangu mwenye nguvu, unikingaye kichwa changu siku ya vita: [8] Ee BWANA, usiwape waovu matakwa yao, usiache mipango yao ikafanikiwa, wasije wakajisifu. [9] Vichwa vya wanaonizunguka vifunikwe na shida zinazosababishwa na midomo yao. [10] Makaa ya mawe ya moto na yawaangukie! Na watupwe motoni, katika mashimo ya matope, wasiinuke tena kamwe. [11] Wasingiziaji wasifanikiwe katika nchi; maafa na yawawinde watu wenye jeuri. [12] Najua kwamba BWANA huwapatia maskini haki, na kuitegemeza njia ya mhitaji. [13] Hakika wenye haki watalisifu jina lako, na waadilifu wataishi mbele zako.