[1] Ee BWANA, ninakuita wewe, uje kwangu hima. Sikia sauti yangu ninapokuita. [2] Maombi yangu na yafike mbele zako kama uvumba; kuinua mikono yangu juu na kuwe kama dhabihu ya jioni. [3] Ee BWANA, weka mlinzi kinywani mwangu, weka ulinzi mlangoni mwa midomo yangu. [4] Usiuache moyo wangu uvutwe katika jambo baya, nisije nikashiriki katika matendo maovu pamoja na watu watendao mabaya, wala nisije nikala vyakula vyao vya anasa. [5] Mtu mwenye haki na anipige: ni jambo la huruma; na anikemee: ni mafuta kichwani mwangu. Kichwa changu hakitalikataa. Hata hivyo, maombi yangu daima ni kinyume cha watenda mabaya, [6] watawala wao watatupwa chini kutoka kwenye majabali, waovu watajifunza kwamba maneno yangu yalikuwa kweli. [7] Watasema, “Kama mtu anavyolima na kuvunja ardhi, ndivyo mifupa yetu imetawanywa kwenye mlango wa kaburi.” [8] Lakini nimekaza macho yangu kwako, Ee BWANA Mwenyezi, ndani yako nimekimbilia, usiniache nife. [9] Niepushe na mitego waliyonitegea, kutokana na mitego iliyotegwa na watenda mabaya. [10] Waovu na waanguke kwenye nyavu zao wenyewe, wakati mimi ninapita salama.