[1] Ee BWANA, umenichunguza na kunijua. [2] Unajua ninapoketi na ninapoinuka; unatambua mawazo yangu tokea mbali. [3] Unafahamu kutoka kwangu na kulala kwangu; unaelewa njia zangu zote. [4] Kabla neno halijafika katika ulimi wangu, wewe walijua kikamilifu, Ee BWANA. [5] Umenizunguka nyuma na mbele; umeweka mkono wako juu yangu. [6] Maarifa haya ni ya ajabu mno kwangu, ni ya juu sana kwangu kuyafikia. [7] Niende wapi nijiepushe na Roho yako? Niende wapi niukimbie uso wako? [8] Kama nikienda juu mbinguni, wewe uko huko; nikifanya vilindi kuwa kitanda changu, wewe uko huko. [9] Kama nikipanda juu ya mbawa za mapambazuko, kama nikikaa pande za mbali za bahari, [10] hata huko mkono wako utaniongoza, mkono wako wa kuume utanishika kwa uthabiti. [11] Kama nikisema, “Hakika giza litanificha na nuru inayonizunguka iwe usiku,” [12] hata giza halitakuwa giza kwako, usiku utangʼaa kama mchana, kwa kuwa giza ni kama nuru kwako. [13] Kwa maana wewe ndiwe uliyeumba utu wangu wa ndani; uliniunga pamoja tumboni mwa mama yangu. [14] Ninakusifu kwa sababu nimeumbwa kwa namna ya ajabu na ya kutisha; kazi zako ni za ajabu, ninajua hayo kikamilifu. [15] Umbile langu halikufichika kwako, nilipoumbwa mahali pa siri. Nilipoungwa pamoja kwa ustadi katika vilindi vya nchi, [16] macho yako yaliniona kabla mwili wangu haujakamilika. Siku zangu zote ulizonipangia ziliandikwa katika kitabu chako kabla haijakuwepo hata moja. [17] Tazama jinsi yalivyo ya thamani mawazo yako kwangu, Ee Mungu! Jinsi jumla yake ilivyo kubwa! [18] Kama ningezihesabu, zingekuwa nyingi kuliko mchanga. Niamkapo, bado niko pamoja nawe. [19] Laiti ungewachinja waovu, Ee Mungu! Ondokeni kwangu, ninyi wamwaga damu! [20] Wanazungumza juu yako wakiwa na kusudi baya, adui zako wanatumia vibaya jina lako. [21] Ee BWANA, je, nisiwachukie wanaokuchukia? Nisiwachukie sana wanaoinuka dhidi yako? [22] Sina kitu zaidi ya chuki dhidi yao, ninawahesabu ni adui zangu. [23] Ee Mungu, nichunguze, uujue moyo wangu, nijaribu na ujue mawazo yangu. [24] Uone kama kuna njia iletayo machukizo ndani yangu, uniongoze katika njia ya milele.