[1] Nitakusifu wewe, Ee BWANA, kwa moyo wangu wote, mbele ya “miungu” nitaimba sifa zako. [2] Nitasujudu nikielekea Hekalu lako takatifu, nami nitalisifu jina lako kwa ajili ya upendo wako na uaminifu, kwa kuwa umelikuza jina lako na neno lako juu ya vitu vyote. [3] Nilipoita, ulinijibu; ulinifanya jasiri na mwenye moyo hodari. [4] Wafalme wote wa dunia wakusifu wewe Ee BWANA, wakati wanaposikia maneno ya kinywa chako. [5] Wao na waimbe kuhusu njia za BWANA, kwa maana utukufu wa BWANA ni mkuu. [6] Ingawa BWANA yuko juu, humwangalia mnyonge, bali mwenye kiburi yeye anamjua kutokea mbali. [7] Nijapopita katikati ya shida, wewe unayahifadhi maisha yangu, unanyoosha mkono wako dhidi ya hasira ya adui zangu, kwa mkono wako wa kuume unaniokoa. [8] BWANA atatimiza kusudi lake kwangu, Ee BWANA, upendo wako wadumu milele: usiziache kazi za mikono yako.