[1] Kando ya mito ya Babeli tuliketi, tukaomboleza tulipokumbuka Sayuni. [2] Kwenye miti ya huko tulitundika vinubi vyetu, [3] kwa maana huko hao waliotuteka walitaka tuwaimbie nyimbo, watesi wetu walidai nyimbo za furaha; walisema, “Tuimbieni wimbo mmoja kati ya nyimbo za Sayuni!” [4] Tutaimbaje nyimbo za BWANA, tukiwa nchi ya kigeni? [5] Nikikusahau wewe, ee Yerusalemu, basi mkono wangu wa kuume na usahau ujuzi wake. [6] Ulimi wangu ushikamane na kaakaa la kinywa changu kama sitakukumbuka wewe, kama nisipokufikiri Yerusalemu kuwa furaha yangu kubwa. [7] Kumbuka, Ee BWANA, walichokifanya Waedomu, siku ile Yerusalemu ilipoanguka. Walisema, “Bomoa, Bomoa mpaka kwenye misingi yake!” [8] Ee binti Babeli, uliyehukumiwa kuangamizwa, heri yeye atakayekulipiza wewe kwa yale uliyotutenda sisi: [9] yeye ambaye atawakamata watoto wako wachanga na kuwaponda juu ya miamba.