Zaburi 119:1-176 ONEN
[1] Heri wale walio waadilifu katika njia zao, wanaoenenda katika sheria ya BWANA. [2] Heri wale wanaozishika shuhuda zake, wamtafutao kwa moyo wao wote. [3] Wasiofanya lolote lililo baya, wanaoenenda katika njia zake. [4] Umetoa maagizo yako ili tuyatii kwa ukamilifu. [5] Laiti mwenendo wangu ungekuwa imara katika kuyatii maagizo yako! [6] Hivyo mimi sitaaibishwa ninapozingatia amri zako zote. [7] Nitakusifu kwa moyo mnyofu ninapojifunza sheria zako za haki. [8] Nitayatii maagizo yako; usiniache kabisa. [9] Kijana aifanye njia yake kuwa safi jinsi gani? Ni kwa kutii, akilifuata neno lako. [10] Ninakutafuta kwa moyo wangu wote, usiniache niende mbali na amri zako. [11] Nimelificha neno lako moyoni mwangu ili nisikutende dhambi. [12] Sifa ni zako, Ee BWANA, nifundishe maagizo yako. [13] Kwa midomo yangu nitasimulia sheria zote zinazotoka katika kinywa chako. [14] Ninafurahia kufuata sheria zako kama mtu afurahiaye mali nyingi. [15] Ninatafakari maagizo yako na kuziangalia njia zako. [16] Ninafurahia maagizo yako, wala sitalipuuza neno lako. [17] Mtendee mema mtumishi wako, nami nitaishi; nitalitii neno lako. [18] Yafungue macho yangu nipate kuona mambo ya ajabu katika sheria yako. [19] Mimi ni mgeni duniani, usinifiche amri zako. [20] Nafsi yangu inataabika kwa shauku kubwa juu ya sheria zako wakati wote. [21] Unawakemea wenye majivuno, waliolaaniwa waendao mbali na amri zako. [22] Niondolee dharau na dhihaka, kwa kuwa ninazishika sheria zako. [23] Ingawa watawala huketi pamoja na kunisingizia, mtumishi wako atatafakari juu ya maagizo yako. [24] Sheria zako ni furaha yangu, nazo ni washauri wangu. [25] Nimelazwa chini mavumbini, yahifadhi maisha yangu sawasawa na neno lako. [26] Nilikueleza njia zangu ukanijibu, nifundishe sheria zako. [27] Nijulishe mafundisho ya mausia yako, nami nitatafakari maajabu yako. [28] Nafsi yangu imechakazwa kwa huzuni, uniimarishe sawasawa na neno lako. [29] Niepushe na njia za udanganyifu, kwa neema unifundishe sheria zako. [30] Nimechagua njia ya kweli, nimekaza moyo wangu katika sheria zako. [31] Nimengʼangʼania sheria zako, Ee BWANA, usiniache niaibishwe. [32] Nakimbilia katika njia ya maagizo yako, kwa kuwa umeuweka moyo wangu huru. [33] Ee BWANA, nifundishe kuyafuata maagizo yako, nami nitayashika mpaka mwisho. [34] Nipe ufahamu, nami nitaishika sheria yako na kuitii kwa moyo wangu wote. [35] Niongoze kwenye njia ya amri zako, kwa kuwa huko napata furaha. [36] Ugeuze moyo wangu kuelekea sheria zako, na siyo kwenye mambo ya ubinafsi. [37] Geuza macho yangu kutoka kwenye mambo yasiyofaa, uyahifadhi maisha yangu sawasawa na neno lako. [38] Mtimizie mtumishi wako ahadi yako, ili upate kuogopwa. [39] Niondolee aibu ninayoiogopa, kwa kuwa sheria zako ni njema. [40] Tazama jinsi ninavyoonea shauku mausia yako! Hifadhi maisha yangu katika haki yako. [41] Ee BWANA, upendo wako usiokoma unijie, wokovu wako sawasawa na ahadi yako, [42] ndipo nitakapomjibu anayenidhihaki, kwa kuwa ninalitumainia neno lako. [43] Usilinyakue neno la kweli kutoka kinywani mwangu, kwa kuwa nimeweka tumaini langu katika amri zako. [44] Nitaitii amri yako daima, naam, milele na milele. [45] Nitatembea nikiwa huru, kwa kuwa nimejifunza mausia yako. [46] Nitasema sheria zako mbele za wafalme wala sitaaibishwa, [47] kwa kuwa ninazifurahia amri zako kwa sababu ninazipenda. [48] Ninaziinulia amri zako ambazo ninazipenda mikono yangu, nami ninatafakari juu ya maagizo yako. [49] Kumbuka neno lako kwa mtumishi wako, kwa sababu umenipa tumaini. [50] Faraja yangu katika mateso yangu ni hii: Ahadi yako inahifadhi maisha yangu. [51] Wenye majivuno wamenisimanga bila kuchoka, hata hivyo sitaiacha sheria yako. [52] Ee BWANA, ninazikumbuka sheria zako za zamani, nazo zinanifariji. [53] Nimeshikwa sana na ghadhabu kwa ajili ya waovu, ambao wameacha sheria yako. [54] Maagizo yako ni kiini cha nyimbo zangu popote ninapoishi. [55] Ee BWANA, wakati wa usiku ninalikumbuka jina lako, nami nitatii sheria yako. [56] Hili limekuwa zoezi langu: nami ninayatii mausia yako. [57] Ee BWANA, wewe ni fungu langu, nimeahidi kuyatii maneno yako. [58] Nimetafuta uso wako kwa moyo wangu wote, nihurumie sawasawa na ahadi yako. [59] Nimezifikiri njia zangu na nimeelekeza hatua zangu katika mausia yako. [60] Nitafanya haraka bila kuchelewa kuzitii amri zako. [61] Hata waovu wanifunge kwa kamba, sitasahau sheria yako. [62] Usiku wa manane ninaamka kukushukuru kwa sababu ya sheria zako za haki. [63] Mimi ni rafiki kwa wale wote wakuchao, kwa wote wanaofuata mausia yako. [64] Ee BWANA, dunia imejaa upendo wako, nifundishe maagizo yako. [65] Mtendee wema mtumishi wako Ee BWANA, sawasawa na neno lako. [66] Nifundishe maarifa na uamuzi mzuri, kwa kuwa ninaamini amri zako. [67] Kabla sijapata shida nilipotea njia, lakini sasa ninalitii neno lako. [68] Wewe ni mwema, unalotenda ni jema, nifundishe maagizo yako. [69] Ingawa wenye majivuno wamenisingizia uongo, nitafuata mausia yako kwa moyo wangu wote. [70] Mioyo yao ni katili na migumu, bali mimi napendezwa na sheria yako. [71] Ilikuwa vyema mimi kupata shida ili nipate kujifunza maagizo yako. [72] Sheria inayotoka kinywani mwako ina thamani kubwa kwangu kuliko maelfu ya vipande vya fedha na dhahabu. [73] Mikono yako ilinifanya na kuniumba, nipe ufahamu niweze kujifunza amri zako. [74] Wakuchao wafurahie wanaponiona, kwa kuwa nimeweka tumaini langu katika neno lako. [75] Ee BWANA, ninajua kwamba sheria zako ni za haki, katika uaminifu wako umeniadhibu. [76] Upendo wako usiokoma uwe faraja yangu, sawasawa na ahadi yako kwa mtumishi wako. [77] Huruma yako na inijie ili nipate kuishi, kwa kuwa naifurahia sheria yako. [78] Wenye majivuno na waaibishwe kwa kunikosea mimi bila sababu, lakini mimi nitatafakari juu ya mausia yako. [79] Wale wakuchao na wanigeukie mimi, hao ambao wanazielewa sheria zako. [80] Moyo wangu usiwe na lawama katika kutii maagizo yako, ili nisiaibishwe. [81] Nafsi yangu inazimia kwa kutamani wokovu wako, lakini nimeweka tumaini langu katika neno lako. [82] Macho yangu yamefifia, nikingoja ahadi yako; ninasema, “Utanifajiri lini?” [83] Ingawa nimekuwa kama kiriba kwenye moshi, bado sijasahau maagizo yako. [84] Mtumishi wako itampasa angoje mpaka lini? Ni lini utawaadhibu washtaki wangu? [85] Wenye majivuno wananichimbia mashimo, kinyume na sheria yako. [86] Amri zako zote ni za kuaminika; unisaidie, kwa sababu watu wananishtaki bila sababu. [87] Walikaribia kabisa kunifuta kutoka uso wa dunia, lakini sijaacha mausia yako. [88] Yahifadhi maisha yangu sawasawa na upendo wako, nami nitatii sheria za kinywa chako. [89] Ee BWANA, neno lako ni la milele, linasimama imara mbinguni. [90] Uaminifu wako unaendelea kwa vizazi vyote, umeiumba dunia, nayo inadumu. [91] Sheria zako zinadumu hadi leo, kwa kuwa vitu vyote vinakutumikia. [92] Kama nisingefurahia sheria yako, ningeangamia katika taabu zangu. [93] Sitasahau mausia yako kamwe, kwa maana kwayo umehifadhi maisha yangu. [94] Uniokoe, kwa maana mimi ni wako, kwa kuwa nimetafuta mausia yako. [95] Waovu wanangojea kuniangamiza, bali mimi ninatafakari sheria zako. [96] Katika ukamilifu wote ninaona mna kikomo, lakini amri zako hazina mpaka. [97] Aha! Tazama, sheria yako naipenda mno ajabu. Ninaitafakari mchana kutwa. [98] Amri zako zimenipa hekima zaidi kuliko adui zangu, kwa kuwa nimezishika daima. [99] Nina akili zaidi kuliko walimu wangu wote, kwa kuwa ninatafakari juu ya sheria zako. [100] Nina ufahamu zaidi kuliko wazee, kwa kuwa ninayatii mausia yako. [101] Nimezuia miguu yangu isiende kwenye kila njia mbaya, ili niweze kutii neno lako. [102] Sijaziacha sheria zako, kwa kuwa umenifundisha wewe mwenyewe. [103] Tazama jinsi maneno yako yalivyo matamu kwangu, matamu kuliko asali katika kinywa changu! [104] Ninapata ufahamu kutoka mausia yako, kwa hiyo ninachukia kila njia ya upotovu. [105] Neno lako ni taa ya miguu yangu na mwanga katika njia yangu. [106] Nimeapa na nimethibitisha, kwamba nitafuata sheria zako za haki. [107] Nimeteseka sana, uhifadhi maisha yangu, Ee BWANA, sawasawa na neno lako. [108] Ee BWANA, pokea sifa za hiari za kinywa changu, nifundishe sheria zako. [109] Ingawa maisha yangu yako hatarini siku zote, sitasahau sheria yako. [110] Waovu wamenitegea mtego, lakini sijayakiuka maagizo yako. [111] Sheria zako ni urithi wangu milele, naam ni furaha ya moyo wangu. [112] Nimekusudia moyoni mwangu kuyafuata maagizo yako mpaka mwisho. [113] Ninachukia watu wa nia mbili, lakini ninapenda sheria yako. [114] Wewe ni kimbilio langu na ngao yangu, nimeweka tumaini langu katika neno lako. [115] Ondokeni kwangu, ninyi mtendao mabaya, ili niweze kushika amri za Mungu wangu! [116] Nihifadhi sawasawa na ahadi yako, nami nitaishi; usiache matumaini yangu yakavunjwa. [117] Nitegemeze, nami nitaokolewa, nami daima nitayaheshimu maagizo yako. [118] Unawakataa wote wanaoyaasi maagizo yako, kwa maana udanganyifu wao ni bure. [119] Waovu wa nchi unawatupa kama takataka, kwa hivyo nazipenda sheria zako. [120] Mwili wangu unatetemeka kwa kukuogopa wewe, ninaziogopa sheria zako. [121] Nimetenda yaliyo haki na sawa, usiniache mikononi mwa watesi wangu. [122] Mhakikishie mtumishi wako usalama, usiache wenye kiburi wanionee. [123] Macho yangu yamefifia, yakitazamia wokovu wako, na kuitazamia ahadi yako ya kweli. [124] Mfanyie mtumishi wako kulingana na upendo wako na unifundishe maagizo yako. [125] Mimi ni mtumishi wako; nipe ufahamu ili niweze kuelewa sheria zako. [126] Ee BWANA, wakati wako wa kutenda umewadia, kwa kuwa sheria yako inavunjwa. [127] Kwa sababu nazipenda amri zako zaidi ya dhahabu, naam, zaidi ya dhahabu safi, [128] na kwa sababu naona maagizo yako yote ni adili, nachukia kila njia potovu. [129] Sheria zako ni za ajabu, hivyo ninazitii. [130] Kuingia kwa maneno yako kunaleta nuru, kunampa mjinga ufahamu. [131] Nimefungua kinywa changu na kuhema, nikitamani amri zako. [132] Nigeukie na unihurumie, kama uwafanyiavyo siku zote wale wanaolipenda jina lako. [133] Ongoza hatua zangu kulingana na neno lako, usiache dhambi yoyote initawale. [134] Niokoe na uonevu wa wanadamu, ili niweze kutii mausia yako. [135] Mwangazie mtumishi wako uso wako na unifundishe amri zako. [136] Chemchemi za machozi zinatiririka kutoka machoni yangu, kwa kuwa sheria yako haifuatwi. [137] Ee BWANA, wewe ni mwenye haki, sheria zako ni sahihi. [138] Sheria ulizoziweka ni za haki, ni za kuaminika kikamilifu. [139] Jitihada yangu imenidhoofisha, kwa kuwa adui zangu wanayapuuza maneno yako. [140] Ahadi zako zimejaribiwa kikamilifu, mtumishi wako anazipenda. [141] Ingawa ni mdogo na ninadharauliwa, sisahau mausia yako. [142] Haki yako ni ya milele, na sheria yako ni kweli. [143] Shida na dhiki zimenipata, lakini amri zako ni furaha yangu. [144] Sheria zako ni sahihi milele, hunipa ufahamu ili nipate kuishi. [145] Ee BWANA, ninakuita kwa moyo wangu wote, nami nitayatii maagizo yako. [146] Ninakuita; niokoe nami nitazishika sheria zako. [147] Ninaamka asubuhi na mapema na kukuomba msaada; nimeweka tumaini langu katika neno lako. [148] Sikufumba macho yangu usiku kucha, ili niweze kutafakari juu ya ahadi zako. [149] Usikie sauti yangu sawasawa na upendo wako, Ee BWANA, uyahifadhi maisha yangu, sawasawa na sheria zako. [150] Wale wanaopanga mipango miovu wako karibu nami, lakini wako mbali na sheria yako. [151] Ee BWANA, hata hivyo wewe u karibu, na amri zako zote ni za kweli. [152] Tangu zamani nimejifunza kutoka shuhuda zako kwamba umezithibitisha ili zidumu milele. [153] Yaangalie mateso yangu, uniokoe, kwa kuwa sijasahau sheria yako. [154] Nitetee katika hali hii yangu na unikomboe, uyahifadhi maisha yangu sawasawa na ahadi yako. [155] Wokovu uko mbali na waovu, kwa kuwa hawatafuti maagizo yako. [156] Ee BWANA, huruma zako ni kuu, uyahifadhi maisha yangu sawasawa na sheria zako. [157] Adui wanaonitesa ni wengi, lakini mimi sitaziacha sheria zako. [158] Ninawatazama wasioamini kwa chuki, kwa kuwa hawalitii neno lako. [159] Tazama jinsi ninavyopenda mausia yako; Ee BWANA, uyahifadhi maisha yangu, sawasawa na upendo wako. [160] Maneno yako yote ni kweli, sheria zako zote za haki ni za milele. [161] Watawala wamenitesa bila sababu, lakini moyo wangu unatetemeka kwa neno lako. [162] Nafurahia ahadi zako kama mtu aliyepata mateka mengi. [163] Ninachukia na kuchukizwa sana na uongo, lakini napenda sheria yako. [164] Ninakusifu mara saba kwa siku, kwa ajili ya sheria zako za haki. [165] Wanaopenda sheria yako wana amani tele, wala hakuna kitu kinachoweza kuwakwaza. [166] Ee BWANA, ninangojea wokovu wako, nami ninafuata amri zako, [167] Ninazitii sheria zako, kwa sababu ninazipenda mno. [168] Nimetii mausia yako na sheria zako, kwa kuwa njia zangu zote zinajulikana kwako. [169] Ee BWANA, kilio changu na kifike mbele zako, nipe ufahamu sawasawa na neno lako. [170] Maombi yangu na yafike mbele zako, niokoe sawasawa na ahadi yako. [171] Midomo yangu na ibubujike sifa, kwa kuwa unanifundisha maagizo yako. [172] Ulimi wangu na uimbe kuhusu neno lako, kwa kuwa amri zako zote ni za haki. [173] Mkono wako uwe tayari kunisaidia, kwa kuwa nimechagua mausia yako. [174] Ee BWANA, ninatamani wokovu wako, na sheria yako ni furaha yangu. [175] Nijalie kuishi ili nipate kukusifu, na sheria zako zinitegemeze. [176] Nimetangatanga kama kondoo aliyepotea. Mtafute mtumishi wako, kwa kuwa sijasahau amri zako.
