Zaburi 118:1-29 ONEN

[1] Mshukuruni BWANA, kwa kuwa ni mwema; upendo wake wadumu milele. [2] Israeli na aseme sasa: “Upendo wake wadumu milele.” [3] Nyumba ya Aroni na iseme sasa: “Upendo wake wadumu milele.” [4] Wote wamchao BWANA na waseme sasa: “Upendo wake wadumu milele.” [5] Wakati wa maumivu yangu makuu nilimlilia BWANA, naye akanijibu kwa kuniweka huru. [6] BWANA yuko pamoja nami, sitaogopa. Mwanadamu anaweza kunitenda nini? [7] BWANA yuko pamoja nami, yeye ni msaidizi wangu. Nitawatazama adui zangu wakiwa wameshindwa. [8] Ni bora kumkimbilia BWANA kuliko kumtumainia mwanadamu. [9] Ni bora kumkimbilia BWANA kuliko kuwatumainia wakuu. [10] Mataifa yote yalinizunguka, lakini kwa jina la BWANA naliwakatilia mbali. [11] Walinizunguka pande zote, lakini kwa jina la BWANA naliwakatilia mbali. [12] Walinizunguka kama kundi la nyuki, lakini walikufa haraka kama miiba iteketeayo; kwa jina la BWANA naliwakatilia mbali. [13] Nilisukumwa nyuma karibu kuanguka, lakini BWANA alinisaidia. [14] BWANA ni nguvu yangu na wimbo wangu, yeye amefanyika wokovu wangu. [15] Sauti za shangwe na ushindi zinavuma hemani mwa wenye haki: “Mkono wa kuume wa BWANA umetenda mambo makuu! [16] Mkono wa kuume wa BWANA umeinuliwa juu, mkono wa kuume wa BWANA umetenda mambo makuu!” [17] Sitakufa, bali nitaishi, nami nitatangaza yale BWANA aliyoyatenda. [18] BWANA ameniadhibu vikali, lakini hakuniacha nife. [19] Nifungulie malango ya haki, nami nitaingia na kumshukuru BWANA. [20] Hili ni lango la BWANA ambalo wenye haki wanaweza kuliingia. [21] Nitakushukuru, kwa kuwa ulinijibu, umekuwa wokovu wangu. [22] Jiwe walilolikataa waashi, limekuwa jiwe kuu la pembeni. [23] BWANA ametenda hili, nalo ni la kushangaza machoni petu. [24] Hii ndiyo siku BWANA aliyoifanya, tushangilie na kufurahi ndani yake. [25] Ee BWANA, tuokoe, Ee BWANA, utujalie mafanikio. [26] Heri yule ajaye kwa jina la BWANA. Kutoka nyumba ya BWANA tunakubariki. [27] BWANA ndiye Mungu, naye ametuangazia nuru yake. Mkiwa na matawi mkononi, unganeni kwenye maandamano ya sikukuu hadi kwenye pembe za madhabahu. [28] Wewe ni Mungu wangu, nitakushukuru, wewe ni Mungu wangu, nitakutukuza. [29] Mshukuruni BWANA kwa kuwa ni mwema; upendo wake wadumu milele.

About this translation

Life Bible app icon
Get the Life Bible app Read offline, sync highlights and notes, and study with your library on any device.