[1] Ee Mungu, moyo wangu ni thabiti; nitaimba na kusifu kwa moyo wangu wote. [2] Amka, kinubi na zeze! Nitayaamsha mapambazuko. [3] Nitakusifu wewe, Ee BWANA, katikati ya mataifa; nitaimba habari zako, katikati ya jamaa za watu. [4] Kwa maana upendo wako ni mkuu, ni juu kuliko mbingu; uaminifu wako unazifikia anga. [5] Ee Mungu, utukuzwe juu ya mbingu, utukufu wako na uenee duniani kote. [6] Tuokoe na utusaidie kwa mkono wako wa kuume, ili wale uwapendao wapate kuokolewa. [7] Mungu amenena kutoka patakatifu pake: “Nitaigawa Shekemu kwa ushindi na kulipima Bonde la Sukothi. [8] Gileadi ni yangu, Manase ni yangu, Efraimu ni kofia yangu ya chuma, nayo Yuda ni fimbo yangu ya utawala. [9] Moabu ni sinia langu la kunawia, juu ya Edomu natupa kiatu changu; nashangilia kwa kushindwa kwa Ufilisti.” [10] Ni nani atakayenipeleka hadi mji wenye ngome? Ni nani atakayeniongoza hadi nifike Edomu? [11] Ee Mungu, si ni wewe uliyetukataa sisi, na hutoki tena na majeshi yetu? [12] Tuletee msaada dhidi ya adui, kwa maana msaada wa mwanadamu haufai kitu. [13] Kwa msaada wa Mungu tutapata ushindi, naye atawaponda adui zetu.