Zaburi 109:1-31 ONEN
[1] Ee Mungu, ambaye ninakusifu, usiwe kimya, [2] kwa maana watu waovu na wadanganyifu wamefungua vinywa vyao dhidi yangu; wasema dhidi yangu kwa ndimi za udanganyifu. [3] Wamenizunguka kwa maneno ya chuki, wananishambulia bila sababu. [4] Wanachonilipa badala ya urafiki wangu ni kunishtaki, lakini mimi ninawaombea. [5] Wananilipiza mabaya kwa mema, chuki badala ya urafiki wangu. [6] Agiza mtu mwovu ampinge, mshtaki asimame mkono wake wa kuume. [7] Anapohukumiwa, apatikane na hatia, nayo maombi yake yamhukumu. [8] Siku zake za kuishi na ziwe chache, nafasi yake ya uongozi ichukuliwe na mtu mwingine. [9] Watoto wake na waachwe yatima, mke wake na awe mjane. [10] Watoto wake na watangetange wakiomba, na wafukuzwe kwenye magofu ya nyumba zao. [11] Mtu anayemdai na ateke vyote alivyo navyo, matunda ya kazi yake yatekwe nyara na wageni. [12] Asiwepo mtu yeyote wa kumtendea mema wala wa kuwahurumia yatima wake. [13] Uzao wake na ukatiliwe mbali, majina yao yafutike katika kizazi kifuatacho. [14] Maovu ya baba zake na yakumbukwe mbele za BWANA, dhambi ya mama yake isifutwe kamwe. [15] Dhambi zao na zibaki daima mbele za BWANA, ili apate kukatilia mbali kumbukumbu lao duniani. [16] Kwa maana kamwe hakuweza kutenda wema, bali alimfukuza mnyonge na mhitaji, aliwafanyia jeuri wahitaji na waliovunjika moyo. [17] Alipenda kulaani, nayo laana ikampata; hakupenda kubariki, kwa hiyo baraka na ikae mbali naye. [18] Alivaa kulaani kama vazi lake, nayo laana ikamwingia mwilini mwake kama maji, kwenye mifupa yake kama mafuta. [19] Na iwe kama joho alilozungushiwa, kama mshipi aliofungiwa daima. [20] Haya na yawe malipo ya BWANA kwa washtaki wangu, kwa wale wanaoninenea mabaya. [21] Lakini wewe, Ee BWANA Mwenyezi, unitendee wema kwa ajili ya jina lako, uniokoe kwa wema wa pendo lako. [22] Maana mimi ni maskini na mhitaji, moyo wangu umejeruhiwa ndani yangu. [23] Ninafifia kama kivuli cha jioni, nimerushwa-rushwa kama nzige. [24] Magoti yangu yamelegea kwa kufunga, mwili wangu umedhoofika na kukonda. [25] Nimekuwa kitu cha kudharauliwa kwa washtaki wangu, wanionapo, hutikisa vichwa vyao. [26] Ee BWANA, Mungu wangu nisaidie, niokoe sawasawa na upendo wako. [27] Watu na wafahamu kuwa ni mkono wako, kwamba wewe, Ee BWANA, umetenda hili. [28] Wanaweza kulaani, lakini wewe utabariki, watakaposhambulia wataaibishwa, lakini mtumishi wako atashangilia. [29] Washtaki wangu watavikwa fedheha, na kufunikwa na aibu kama joho. [30] Kwa kinywa changu nitamtukuza sana BWANA, katika umati mkubwa nitamsifu. [31] Kwa maana husimama mkono wa kuume wa mhitaji, kuokoa maisha yake kutoka kwa wale wanaomhukumu.
