Zaburi 107:1-43 ONEN
[1] Mshukuruni BWANA, kwa kuwa yeye ni mwema, upendo wake wadumu milele. [2] Waliokombolewa wa BWANA na waseme hivi, wale aliowaokoa kutoka mkono wa adui, [3] wale aliowakusanya kutoka nchi mbalimbali, kutoka mashariki na magharibi, kutoka kaskazini na kusini. [4] Baadhi yao walitangatanga jangwani, hawakuona njia ya kuwafikisha mji ambao wangeweza kuishi. [5] Walikuwa na njaa na kiu, nafsi zao zikadhoofika. [6] Ndipo walipomlilia BWANA katika shida yao, naye akawaokoa kutoka taabu yao. [7] Akawaongoza kwa njia iliyo sawa hadi mji ambao wangeweza kuishi. [8] Basi na wamshukuru BWANA kwa upendo wake usiokoma, na kwa matendo yake ya ajabu kwa wanadamu, [9] kwa maana yeye humtosheleza mwenye kiu, na kumshibisha mwenye njaa kwa vitu vyema. [10] Wengine walikaa gizani na katika huzuni kuu, wafungwa wakiteseka katika minyororo, [11] kwa sababu walikuwa wameasi dhidi ya maneno ya Mungu na kudharau shauri la Aliye Juu Sana. [12] Aliwatumikisha kwa kazi ngumu; walijikwaa na hapakuwepo yeyote wa kuwasaidia. [13] Ndipo walipomlilia BWANA katika shida yao, naye akawaokoa kutoka taabu yao. [14] Akawatoa katika giza na huzuni kuu na akavunja minyororo yao. [15] Basi na wamshukuru BWANA kwa upendo wake usiokoma, na kwa matendo yake ya ajabu kwa wanadamu, [16] kwa kuwa yeye huvunja malango ya shaba na kukata mapingo ya chuma. [17] Wengine wakawa wapumbavu kutokana na uasi wao, wakapata mateso kwa sababu ya uovu wao. [18] Wakachukia kabisa vyakula vyote, wakakaribia malango ya mauti. [19] Ndipo walipomlilia BWANA katika shida yao, naye akawaokoa kutoka taabu yao. [20] Akalituma neno lake na kuwaponya, akawaokoa kutoka maangamizo yao. [21] Basi na wamshukuru BWANA kwa upendo wake usiokoma, na kwa matendo yake ya ajabu kwa wanadamu. [22] Na watoe dhabihu za kushukuru, na wasimulie matendo yake kwa nyimbo za furaha. [23] Wengine walisafiri baharini kwa meli, walikuwa wafanyabiashara kwenye maji makuu. [24] Waliziona kazi za BWANA, matendo yake ya ajabu kilindini. [25] Kwa maana alisema na kuamsha tufani iliyoinua mawimbi juu. [26] Yakainuka juu mbinguni, yakashuka chini hadi vilindini, katika hatari hii ujasiri wao uliyeyuka. [27] Walipepesuka na kuyumbayumba kama walevi, ujanja wao ukafikia ukomo. [28] Ndipo walipomlilia BWANA katika shida yao, naye akawatoa kwenye taabu yao. [29] Akatuliza dhoruba kwa mnongʼono, mawimbi ya bahari yakatulia. [30] Walifurahi ilipokuwa shwari, naye akawaongoza hadi bandari waliyoitamani. [31] Basi na wamshukuru BWANA kwa upendo wake usiokoma, na kwa matendo yake ya ajabu kwa wanadamu. [32] Na wamtukuze yeye katika kusanyiko la watu, na wamsifu katika baraza la wazee. [33] Yeye aligeuza mito kuwa jangwa, chemchemi za maji zitiririkazo kuwa ardhi yenye kiu, [34] nchi izaayo ikawa ya chumvi isiyofaa, kwa sababu ya uovu wa wale walioishi humo. [35] Aligeuza jangwa likawa madimbwi ya maji, nayo ardhi kame kuwa chemchemi za maji zitiririkazo; [36] aliwaleta wenye njaa wakaishi humo, nao wakajenga mji wangeweza kuishi. [37] Walilima mashamba na kupanda mizabibu, nayo ikazaa matunda mengi, [38] Mungu aliwabariki, hesabu yao ikaongezeka sana, wala hakuruhusu mifugo yao kupungua. [39] Kisha hesabu yao ilipungua, na walinyenyekeshwa kwa kuonewa, maafa na huzuni. [40] Yeye ambaye huwamwagia dharau wakuu, aliwafanya watangetange nyikani isiyo na njia. [41] Lakini yeye aliwainua wahitaji katika taabu zao, na kuongeza jamaa zao kama makundi ya kondoo. [42] Wanyofu wataona na kufurahi, lakini waovu wote watafunga vinywa vyao. [43] Yeyote aliye na hekima, ayasikie mambo haya, na atafakari upendo mkuu wa BWANA.
