Zaburi 106:1-48 ONEN
[1] Msifuni BWANA. Mshukuruni BWANA, kwa kuwa ni mwema; upendo wake wadumu milele. [2] Ni nani awezaye kusimulia matendo makuu ya BWANA au kutangaza kikamilifu sifa zake? [3] Heri wale wanaodumisha haki, ambao daima wanafanya yaliyo mema. [4] Ee BWANA, unikumbuke unapowatendea mema watu wako, uwe msaada wangu unapowaokoa, [5] ili niweze kufurahia mafanikio ya wateule wako, niweze kushiriki katika furaha ya taifa lako, na kuungana na urithi wako katika kukusifu. [6] Tumetenda dhambi, kama vile baba zetu walivyotenda, tumekosa na tumetenda uovu. [7] Wakati baba zetu walipokuwa Misri, hawakuzingatia maajabu yako, wala hawakukumbuka wingi wa fadhili zako, bali waliasi kando ya bahari, Bahari ya Shamu. [8] Hata hivyo aliwaokoa kwa ajili ya jina lake, ili apate kudhihirisha uweza wake mkuu. [9] Alikemea Bahari ya Shamu, nayo ikakauka, akawaongoza katika vilindi vyake kama vile jangwani. [10] Aliwaokoa mikononi mwa adui; kutoka mikononi mwa adui aliwakomboa. [11] Maji yaliwafunika adui zao, hakunusurika hata mmoja. [12] Ndipo walipoamini ahadi zake, nao wakaimba sifa zake. [13] Lakini mara walisahau aliyowatendea, wala hawakungojea shauri lake. [14] Jangwani walitawaliwa na tamaa zao, walimjaribu Mungu nyikani. [15] Kwa hiyo aliwapa kile walichoomba, lakini akatuma juu yao ugonjwa wa kudhoofisha. [16] Kambini walimwonea wivu Mose, na pia Aroni aliyekuwa amewekwa wakfu kwa BWANA. [17] Ardhi ilifunguka ikawameza Dathani, ikawazika Abiramu na kundi lake. [18] Moto uliwaka katikati ya wafuasi wao, mwali wa moto uliwateketeza waovu. [19] Huko Horebu walitengeneza ndama, na kuabudu sanamu ya kusubu kwa chuma. [20] Waliubadilisha Utukufu wao kwa sanamu ya fahali, ambaye hula majani. [21] Walimsahau Mungu aliyewaokoa, aliyekuwa ametenda mambo makuu huko Misri, [22] miujiza katika nchi ya Hamu na mambo ya kutisha huko Bahari ya Shamu. [23] Kwa hiyo alisema kwamba angewaangamiza: kama Mose mteule wake, asingesimama kati yao na Mungu kuizuia ghadhabu yake kuwaangamiza. [24] Kisha waliidharau ile nchi nzuri, hawakuiamini ahadi yake. [25] Walinungʼunika ndani ya mahema yao, wala hawakumtii BWANA. [26] Kwa hiyo akaapa kwa mkono ulioinuliwa kwamba atawafanya waanguke jangwani, [27] kuwatawanya wazao wao waanguke miongoni mwa mataifa, na kuwatawanya katika nchi zote. [28] Walijifunga nira na Baali wa Peori, wakala dhabihu zilizotolewa kwa miungu isiyo na uhai. [29] Waliichochea hasira ya BWANA, wakamkasirisha kwa matendo yao maovu, nayo tauni ikazuka katikati yao. [30] Lakini Finehasi alisimama na kuingilia kati, nayo tauni ikazuiliwa. [31] Hili likahesabiwa kwake haki, kwa vizazi visivyo na mwisho vijavyo. [32] Kwenye maji ya Meriba, walimkasirisha BWANA, janga likampata Mose kwa sababu yao; [33] kwa maana walimwasi Roho wa Mungu, na maneno yasiyofaa yakatoka midomoni kwa Mose. [34] Hawakuyaangamiza yale mataifa kama BWANA alivyowaagiza, [35] bali walijichanganya na mataifa na wakazikubali desturi zao. [36] Waliabudu sanamu zao, zikawa mtego kwao. [37] Wakawatoa wana wao na binti zao dhabihu kwa mashetani. [38] Walimwaga damu isiyo na hatia, damu za wana wao na binti zao, ambao waliwatoa dhabihu kwa sanamu za Kanaani, nayo nchi ikanajisika kwa damu zao. [39] Wakajinajisi wenyewe kwa yale waliyotenda; kwa matendo yao wenyewe wakajifanyia ukahaba. [40] Kwa hiyo BWANA akawakasirikia watu wake na akauchukia sana urithi wake. [41] Akawakabidhi kwa mataifa na adui zao wakawatawala. [42] Adui zao wakawaonea na kuwatia chini ya mamlaka yao. [43] Mara nyingi aliwaokoa lakini walikuwa wamezama kwenye uasi, nao wakajiharibu katika dhambi zao. [44] Lakini akaangalia mateso yao wakati aliposikia kilio chao; [45] kwa ajili yao akakumbuka agano lake, na kutokana na upendo wake mkuu akapooza hasira yake. [46] Akawafanya wahurumiwe na wote waliowashikilia mateka. [47] Ee BWANA Mungu wetu, tuokoe. Tukusanye tena kutoka kwa mataifa, ili tuweze kulishukuru jina lako takatifu, na kushangilia katika sifa zako. [48] Atukuzwe BWANA, Mungu wa Israeli, tangu milele na hata milele. Watu wote na waseme, “Amen!” Msifuni BWANA.
