Zaburi 105:1-45 ONEN
[1] Mshukuruni BWANA, liitieni jina lake, wajulisheni mataifa yale aliyoyatenda. [2] Mwimbieni yeye, mwimbieni yeye sifa, waambieni matendo yake yote ya ajabu. [3] Lishangilieni jina lake takatifu, mioyo ya wale wamtafutao BWANA na ifurahi. [4] Mtafuteni BWANA na nguvu zake, utafuteni uso wake siku zote. [5] Kumbuka matendo ya ajabu aliyoyafanya, miujiza yake na hukumu alizozitamka, [6] enyi wazao wa Abrahamu mtumishi wake, enyi wana wa Yakobo, wateule wake. [7] Yeye ndiye BWANA Mungu wetu, hukumu zake zimo duniani pote. [8] Hulikumbuka agano lake milele, neno ambalo aliamuru, kwa vizazi elfu, [9] agano alilolifanya na Abrahamu, kiapo alichomwapia Isaki. [10] Alilithibitisha kwa Yakobo kuwa amri, kwa Israeli liwe agano la milele: [11] “Nitakupa wewe nchi ya Kanaani kuwa sehemu utakayoirithi.” [12] Walipokuwa wachache kwa idadi, wachache sana na wageni ndani yake, [13] walitangatanga kutoka taifa moja hadi jingine, kutoka ufalme mmoja hadi mwingine. [14] Hakuruhusu mtu yeyote awaonee; kwa ajili yao aliwakemea wafalme, akisema: [15] “Msiwaguse niliowatia mafuta; msiwadhuru manabii wangu.” [16] Akaiita njaa juu ya nchi na kuharibu chakula chao chote, [17] naye akatuma mtu mbele yao, Yosefu, aliyeuzwa kama mtumwa. [18] Walichubua miguu yake kwa minyororo, shingo yake ilifungwa kwa chuma, [19] hadi yale aliyotangulia kusema yalipotimia, hadi neno la BWANA lilipomthibitisha. [20] Mfalme alituma watu wakamfungua, mtawala wa watu alimwachia huru. [21] Alimfanya mkuu wa nyumba yake, mtawala juu ya vyote alivyokuwa navyo, [22] kuwaelekeza wakuu wa mfalme apendavyo na kuwafundisha wazee wake hekima. [23] Kisha Israeli akaingia Misri, Yakobo akaishi kama mgeni katika nchi ya Hamu. [24] BWANA aliwafanya watu wake kuzaana sana, akawafanya kuwa wengi sana kuliko adui zao, [25] ndiye aliigeuza mioyo yao iwachukie watu wake, wakatenda hila dhidi ya watumishi wake. [26] Akamtuma Mose mtumishi wake, pamoja na Aroni, aliyemchagua. [27] Walifanya ishara zake za ajabu miongoni mwao, miujiza yake katika nchi ya Hamu. [28] Alituma giza na nchi ikajaa giza, kwani si walikuwa wameyaasi maneno yake? [29] Aligeuza maji yao kuwa damu, ikasababisha samaki wao kufa. [30] Nchi yao ilijaa vyura tele, ambao waliingia hadi kwenye vyumba vya kulala vya watawala wao. [31] Alisema, yakaja makundi ya mainzi, na viroboto katika nchi yao yote. [32] Alibadilisha mvua yao ikawa mvua ya mawe, yenye umeme wa radi nchini yao yote, [33] akaharibu mizabibu yao na miti ya tini, na akaangamiza miti ya nchi yao. [34] Alisema, nzige wakaja, tunutu wasio na idadi, [35] wakala kila jani katika nchi yao, wakala mazao ya ardhi yao. [36] Kisha akawaua wazaliwa wote wa kwanza katika nchi yao, matunda ya kwanza ya ujana wao wote. [37] Akawatoa Israeli katika nchi wakiwa na fedha na dhahabu nyingi, wala hakuna hata mmoja kutoka kabila zao aliyejikwaa. [38] Misri ilifurahi walipoondoka, kwa sababu hofu ya Israeli ilikuwa imewaangukia. [39] Alitandaza wingu kama kifuniko, na moto kuwamulikia usiku. [40] Waliomba, naye akawaletea kware, akawashibisha kwa mkate wa mbinguni. [41] Alipasua mwamba, maji yakabubujika, yakatiririka jangwani kama mto. [42] Kwa maana alikumbuka ahadi yake takatifu, aliyompa Abrahamu mtumishi wake. [43] Aliwatoa watu wake kwa furaha, wateule wake kwa kelele za shangwe, [44] akawapa nchi za mataifa, wakawa warithi wa mali wengine walikuwa wameitaabikia: [45] alifanya haya ili wayashike mausia yake na kuzitii sheria zake. Msifuni BWANA.
