Zaburi 104:1-35 ONEN
[1] Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA. Ee BWANA Mungu wangu, wewe ni mkuu sana, umejivika utukufu na enzi. [2] Amejifunika katika nuru kama vile kwa vazi, amezitandaza mbingu kama hema [3] na kuziweka nguzo za orofa yake juu ya maji. Huyafanya mawingu kuwa gari lake, na hupanda kwenye mbawa za upepo. [4] Huzifanya pepo kuwa wajumbe wake, miali ya moto watumishi wake. [5] Ameiweka dunia kwenye misingi yake, haiwezi kamwe kuondoshwa. [6] Uliifunika kwa kilindi kama kwa vazi, maji yalisimama juu ya milima. [7] Lakini kwa kukemea kwako maji yalikimbia, kwa sauti ya radi yako yakatoroka, [8] yakapanda milima, yakateremka mabondeni, hadi mahali pale ulipoyakusudia. [9] Uliyawekea mpaka ambao hayawezi kuuvuka, kamwe hayataifunika dunia tena. [10] Huzifanya chemchemi zimwage maji mabondeni, hutiririka kati ya milima. [11] Huwapa maji wanyama wote wa kondeni, punda-mwitu huzima kiu yao. [12] Ndege wa angani hufanya viota kando ya maji, huimba katikati ya matawi. [13] Huinyeshea milima kutoka orofa zake, dunia inatoshelezwa kwa matunda ya kazi yake. [14] Huyafanya majani ya mifugo yaote, na mimea kwa watu kulima, wajipatie chakula kutoka ardhini: [15] divai ya kuufurahisha moyo wa mwanadamu, mafuta kwa ajili ya kungʼarisha uso wake, na mkate wa kutia mwili nguvu. [16] Miti ya BWANA inanyeshewa vizuri, mierezi ya Lebanoni aliyoipanda. [17] Humo ndege hufanya viota vyao, korongo ana nyumba yake kwenye msunobari. [18] Milima mirefu ni makao ya mbuzi-mwitu, majabali ni kimbilio la pelele. [19] Mwezi hugawanya majira, na jua hutambua wakati wake wa kutua. [20] Unaleta giza, kunakuwa usiku, wanyama wote wa mwituni huzurura. [21] Simba hunguruma kwa mawindo yao, na kutafuta chakula chao kutoka kwa Mungu. [22] Jua huchomoza, nao huondoka, hurudi na kulala katika mapango yao. [23] Kisha mwanadamu huenda kazini mwake, katika kazi yake mpaka jioni. [24] Ee BWANA, jinsi matendo yako yalivyo mengi! Kwa hekima ulizifanya zote, dunia imejaa viumbe vyako. [25] Pale kuna bahari, kubwa na yenye nafasi tele, imejaa viumbe visivyo na idadi, vitu vyenye uhai vikubwa na vidogo. [26] Huko meli huenda na kurudi, pia Lewiathani, uliyemuumba acheze ndani yake. [27] Hawa wote wanakutazamia wewe, uwape chakula chao kwa wakati wake. [28] Wakati unapowapa, wanakikusanya, unapofumbua mkono wako, wao wanashibishwa mema. [29] Unapoficha uso wako, wanapata hofu, unapoondoa pumzi yao, wanakufa na kurudi mavumbini. [30] Unapopeleka Roho wako, wanaumbwa, nawe huufanya upya uso wa dunia. [31] Utukufu wa BWANA na udumu milele, BWANA na azifurahie kazi zake: [32] yeye aitazamaye dunia, nayo ikatetemeka, aigusaye milima, nayo ikatoa moshi. [33] Nitamwimbia BWANA maisha yangu yote; nitaimba sifa kwa Mungu wangu muda wote ninaoishi. [34] Kutafakari kwangu na kumpendeze yeye, ninapofurahi katika BWANA. [35] Lakini wenye dhambi na watoweke katika dunia na waovu wasiwepo tena. Ee nafsi yangu, msifu BWANA. Msifuni BWANA.
