[1] Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA. Vyote vilivyomo ndani yangu vilihimidi jina lake takatifu. [2] Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA, wala usisahau wema wake wote, [3] akusamehe dhambi zako zote, akuponya magonjwa yako yote, [4] aukomboa uhai wako na kaburi, akuvika taji ya upendo na huruma, [5] atosheleza mahitaji yako kwa vitu vyema, ili ujana wako uhuishwe kama wa tai. [6] BWANA hutenda haki, naye huwapa hukumu ya haki wote wanaoonewa. [7] Alijulisha Mose njia zake, na wana wa Israeli matendo yake. [8] BWANA ni mwingi wa huruma na mwenye neema; si mwepesi wa hasira, bali amejaa upendo. [9] Yeye hatalaumu siku zote, wala haweki hasira yake milele, [10] yeye hatutendei kulingana na dhambi zetu wala hatupatilizi kwa kadiri ya maovu yetu. [11] Kama vile mbingu zilivyo juu ya dunia sana, ndivyo wema wake ulivyo mwingi kwa wanaomcha; [12] kama mashariki ilivyo mbali na magharibi, ndivyo Mungu alivyoziweka dhambi zetu mbali nasi. [13] Kama baba alivyo na huruma kwa watoto wake, ndivyo BWANA anavyowahurumia wale wanaomcha; [14] kwa kuwa anajua tulivyoumbwa, anakumbuka kwamba sisi tu mavumbi. [15] Kuhusu mwanadamu, siku zake ni kama majani, anachanua kama ua la shambani; [16] upepo huvuma juu yake nalo hutoweka, mahali pake hapalikumbuki tena. [17] Lakini kutoka milele hata milele upendo wa BWANA uko kwa wale wamchao, nayo haki yake kwa watoto wa watoto wao: [18] kwa wale walishikao agano lake na kukumbuka kuyatii mausia yake. [19] BWANA ameweka imara kiti chake cha enzi mbinguni, ufalme wake unatawala juu ya vyote. [20] Mhimidini BWANA, enyi malaika zake, ninyi mlio mashujaa mnaozitii amri zake, ninyi mnaotii neno lake. [21] Mhimidini BWANA, ninyi jeshi lake lote la mbinguni, ninyi watumishi wake mnaofanya mapenzi yake. [22] Mhimidini BWANA, kazi zake zote kila mahali katika milki yake. Ee nafsi yangu, umhimidi BWANA.