[1] Ee BWANA, usikie maombi yangu, kilio changu cha kuomba msaada kikufikie. [2] Usinifiche uso wako ninapokuwa katika shida. Unitegee sikio lako, ninapoita, unijibu kwa upesi. [3] Kwa kuwa siku zangu zinatoweka kama moshi, mifupa yangu inaungua kama kaa la moto. [4] Moyo wangu umefifia na kunyauka kama jani, ninasahau kula chakula changu. [5] Kwa sababu ya kusononeka kwangu kwa uchungu, nimebakia ngozi na mifupa. [6] Nimekuwa kama bundi wa jangwani, kama bundi kwenye magofu. [7] Nilalapo sipati usingizi, nimekuwa kama ndege mpweke kwenye paa la nyumba. [8] Mchana kutwa adui zangu hunidhihaki, wale wanaonizunguka hutumia jina langu kama laana. [9] Ninakula majivu kama chakula changu na nimechanganya kinywaji changu na machozi [10] kwa sababu ya ghadhabu yako kuu, kwa maana umeniinua na kunitupa kando. [11] Siku zangu ni kama kivuli cha jioni, ninanyauka kama jani. [12] Lakini wewe, Ee BWANA, umeketi katika kiti chako cha enzi milele, sifa zako za ukuu zaendelea vizazi vyote. [13] Utainuka na kuihurumia Sayuni, kwa maana ni wakati wa kumwonyesha wema; wakati uliokubalika umewadia. [14] Kwa maana mawe yake ni ya thamani kwa watumishi wako, vumbi lake lenyewe hulionea huruma. [15] Mataifa wataogopa jina la BWANA, wafalme wote wa dunia watauheshimu utukufu wako. [16] Kwa maana BWANA ataijenga tena Sayuni na kutokea katika utukufu wake. [17] Ataitikia maombi ya mtu mkiwa, wala hatadharau hoja yao. [18] Hili na liandikwe kwa ajili ya kizazi kijacho, ili taifa litakaloumbwa baadaye waweze kumsifu BWANA: [19] “BWANA alitazama chini kutoka patakatifu pake palipo juu, kutoka mbinguni alitazama dunia, [20] kusikiliza vilio vya uchungu vya wafungwa na kuwaweka huru wale waliohukumiwa kufa.” [21] Kwa hiyo jina la BWANA latangazwa huko Sayuni na sifa zake katika Yerusalemu, [22] wakati mataifa na falme zitakapokusanyika ili kumwabudu BWANA. [23] Katika kuishi kwangu alivunja nguvu zangu, akafupisha siku zangu. [24] Ndipo niliposema: “Ee Mungu wangu, usinichukue katikati ya siku zangu; miaka yako inaendelea vizazi vyote. [25] Hapo mwanzo uliweka misingi ya dunia, nazo mbingu ni kazi ya mikono yako. [26] Hizi zitatoweka, lakini wewe utadumu, zote zitachakaa kama vazi. Utazibadilisha kama nguo nazo zitaondoshwa. [27] Lakini wewe, U yeye yule, nayo miaka yako haikomi kamwe. [28] Watoto wa watumishi wako wataishi mbele zako; wazao wao wataimarishwa mbele zako.”