[1] Kwa nini, Ee BWANA, unasimama mbali? Kwa nini unajificha wakati wa shida? [2] Katika kiburi chake, mwovu humtesa maskini, waovu na wanaswe katika hila wanazozitunga. [3] Hujivunia tamaa za moyo wake; humbariki mlafi na kumtukana BWANA. [4] Katika kiburi chake, mwovu hamtafuti Mungu, katika mawazo yake yote hakuna nafasi ya Mungu. [5] Njia zake daima hufanikiwa; hujivuna na amri zako ziko mbali naye, huwacheka kwa dharau adui zake wote. [6] Anajisemea mwenyewe, “Hakuna kitakachonitikisa, daima nitakuwa na furaha, kamwe sitakuwa na shida.” [7] Kinywa chake kimejaa laana, uongo na vitisho; shida na ubaya viko chini ya ulimi wake. [8] Huvizia karibu na vijiji; kutoka mafichoni huwanasa wasio na hatia, akivizia wapitaji. [9] Huvizia kama simba aliye mawindoni; huvizia kumkamata mnyonge, huwakamata wanyonge na kuwaburuza katika wavu wake. [10] Mateka wake hupondwa, huzimia; wanaanguka katika nguvu zake. [11] Anajisemea mwenyewe, “Mungu amesahau, huficha uso wake na haoni kabisa.” [12] Inuka BWANA! Inua mkono wako, Ee Mungu. Usiwasahau wanyonge. [13] Kwa nini mtu mwovu anamtukana Mungu? Kwa nini anajiambia mwenyewe, “Hataniita nitoe hesabu?” [14] Lakini wewe, Ee Mungu, unaona shida na huzuni, umekubali kuyapokea mkononi mwako. Mhanga anajisalimisha kwako, wewe ni msaada wa yatima. [15] Vunja mkono wa mtu mwovu na mbaya, mwite atoe hesabu ya maovu yake ambayo yasingejulikana. [16] BWANA ni Mfalme milele na milele, mataifa wataangamia watoke nchini mwake. [17] Unasikia, Ee BWANA, shauku ya wanaoonewa, wewe huwatia moyo, na kusikiliza kilio chao, [18] ukiwatetea yatima na walioonewa, ili mwanadamu, ambaye ni udongo, asiogopeshe tena.