[1] Ee BWANA, nitakutukuza kwa moyo wangu wote, nitayasimulia matendo yako yote ya ajabu. [2] Nitafurahi na kushangilia ndani yako. Nitaliimbia sifa jina lako, Ewe Uliye Juu Sana. [3] Adui zangu wamerudi nyuma, wamejikwaa na kuangamia mbele zako. [4] Kwa maana umetetea haki yangu na msimamo wangu; umeketi kwenye kiti chako cha enzi, ukihukumu kwa haki. [5] Umekemea mataifa na kuwaangamiza waovu; umeyafuta majina yao milele na milele. [6] Uharibifu usiokoma umempata adui, umeingʼoa miji yao; hata kumbukumbu lao limetoweka. [7] BWANA anatawala milele, ameweka kiti chake cha enzi apate kuhukumu. [8] Mungu atahukumu ulimwengu kwa haki, atatawala mataifa kwa haki. [9] BWANA ni kimbilio la watu wanaoonewa, ni ngome imara wakati wa shida. [10] Wote wanaolijua jina lako watakutumaini wewe, kwa maana wewe BWANA, hujawaacha kamwe wakutafutao. [11] Mwimbieni BWANA sifa, amefanywa mtawala Sayuni, tangazeni miongoni mwa mataifa, yale aliyoyatenda. [12] Kwa maana yeye alipizaye kisasi cha damu hukumbuka, hapuuzi kilio cha wanaoonewa. [13] Ee BWANA, tazama jinsi walivyo wengi adui zangu wanaonitesa! Nihurumie, uniinue kutoka malango ya mauti, [14] ili niweze kutangaza sifa zako katika malango ya Binti Sayuni na huko niushangilie wokovu wako. [15] Mataifa wameanguka kwenye shimo walilolichimba, miguu yao imenaswa kwenye wavu waliouficha. [16] BWANA anajulikana kwa haki yake, waovu wamenaswa katika kazi za mikono yao. [17] Waovu wataishia kuzimu, naam, mataifa yote wanaomsahau Mungu. [18] Lakini mhitaji hatasahaulika siku zote, wala matumaini ya walioonewa hayatapotea. [19] Ee BWANA, inuka, usimwache binadamu ashinde. Mataifa na yahukumiwe mbele zako. [20] Ee BWANA, wapige kwa hofu, mataifa na yajue kuwa wao ni watu tu.