[1] Ee binti wa mwana wa mfalme, tazama jinsi inavyopendeza miguu yako katika viatu! Miguu yako yenye madaha ni kama vito vya thamani, kazi ya mikono ya fundi stadi. [2] Kitovu chako ni kama bilauri ya mviringo ambayo kamwe haikosi divai iliyochanganywa. Kiuno chako ni kichuguu cha ngano kilichozungukwa kwa yungiyungi. [3] Matiti yako ni kama wana-paa wawili, mapacha wa paa. [4] Shingo yako ni kama mnara wa pembe ya ndovu. Macho yako ni vidimbwi vya Heshboni karibu na lango la Beth-Rabi. Pua lako ni kama mnara wa Lebanoni ukitazama kuelekea Dameski. [5] Kichwa chako kinakuvika taji kama mlima Karmeli. Nywele zako ni kama zulia la urujuani; mfalme ametekwa na mashungi yake. [6] Tazama jinsi ulivyo mzuri na unavyopendeza, ee pendo, kwa uzuri wako! [7] Umbo lako ni kama la mtende, nayo matiti yako kama vishada vya matunda. [8] Nilisema, “Nitakwea mtende, nami nitayashika matunda yake.” Matiti yako na yawe kama vishada vya mzabibu, harufu nzuri ya pumzi yako kama matofaa, [9] na kinywa chako kama divai bora kuliko zote. Divai na iende moja kwa moja hadi kwa mpenzi wangu, ikitiririka polepole juu ya midomo na meno. [10] Mimi ni mali ya mpenzi wangu, nayo shauku yake ni juu yangu. [11] Njoo, mpenzi wangu, twende mashambani, twende tukalale huko vijijini. [12] Hebu na twende mapema katika mashamba ya mizabibu tuone kama mizabibu imechipua, kama maua yake yamefunguka, na kama mikomamanga imetoa maua: huko nitakupa penzi langu. [13] Mitunguja hutoa harufu zake nzuri, kwenye milango yetu kuna matunda mazuri, mapya na ya zamani, ambayo nimekuhifadhia wewe, mpenzi wangu.