[1] Mpenzi wako amekwenda wapi, ewe mzuri kupita wanawake wote? Mpenzi wako amegeukia njia ipi, tupate kumtafuta pamoja nawe? [2] Mpenzi wangu amekwenda bustanini mwake, kwenye vitalu vya vikolezo, kujilisha bustanini na kukusanya yungiyungi. [3] Mimi ni wake mpenzi wangu, na mpenzi wangu ni wangu; yeye hujilisha katikati ya yungiyungi. [4] Wewe ni mzuri, mpenzi wangu, kama Tirsa, upendezaye kama Yerusalemu, umetukuka kama jeshi lenye bendera. [5] Uyageuze macho yako mbali nami, yananigharikisha. Nywele zako ni kama kundi la mbuzi wanaoteremka kutoka Gileadi. [6] Meno yako ni kama kundi la kondoo watokao kuogeshwa. Kila mmoja ana pacha lake, hakuna hata mmoja aliye peke yake. [7] Mashavu yako nyuma ya shela yako ni kama vipande viwili vya komamanga. [8] Panaweza kuwepo malkia sitini, masuria themanini na mabikira wasiohesabika; [9] lakini hua wangu, mkamilifu wangu, ni wa namna ya pekee, binti pekee kwa mama yake, kipenzi cha yeye aliyemzaa. Wanawali walimwona na kumwita aliyebarikiwa; malkia na masuria walimsifu. [10] Ni nani huyu atokeaye kama mapambazuko, mzuri kama mwezi, mwangavu kama jua, ametukuka kama nyota zifuatanazo? [11] Niliteremka kwenye bustani ya miti ya milozi ili kutazama machipuko ya bondeni, kuona kama mizabibu imechipua au kama mikomamanga imechanua maua. [12] Kabla sijangʼamua, shauku yangu iliniweka katikati ya magari ya kifalme ya kukokotwa na farasi ya watu wangu. [13] Rudi, rudi, ee Mshulami; rudi, rudi ili tupate kukutazama! Kwa nini kumtazama Mshulami, kama kutazama ngoma ya Mahanaimu?