[1] Laiti ungelikuwa kwangu kama ndugu wa kiume, ambaye aliyanyonya matiti ya mama yangu! Kisha, kama ningekukuta huko nje, ningelikubusu, wala hakuna mtu yeyote angelinidharau. [2] Ningelikuongoza na kukuleta katika nyumba ya mama yangu, yeye ambaye amenifundisha. Ningelikupa divai iliyokolezwa unywe, asali ya maua ya mikomamanga yangu. [3] Mkono wake wa kushoto uko chini ya kichwa changu, na mkono wake wa kuume unanikumbatia. [4] Binti za Yerusalemu, ninawaagiza: msichochee wala kuamsha mapenzi hata yatakapotaka yenyewe. [5] Ni nani huyu anayekuja kutoka nyikani akimwegemea mpenzi wake? Nilikuamsha chini ya mtofaa, huko mama yako alipotunga mimba yako, huko yeye alipata utungu akakuzaa. [6] Nitie kama muhuri moyoni mwako, kama muhuri kwenye mkono wako; kwa maana upendo una nguvu kama mauti, wivu wake ni mkatili kama kuzimu. Unachoma kama mwali wa moto, kama mwali mkubwa wa moto wa BWANA hasa. [7] Maji mengi hayawezi kuuzimisha upendo, mito haiwezi kuugharikisha. Kama mtu angelitoa mali yote ya nyumbani mwake kwa ajili ya upendo, angelidharauliwa kabisa. [8] Tunaye dada mdogo, matiti yake hayajakua bado. Tutafanya nini kwa ajili ya dada yetu wakati atakapokuja kuposwa? [9] Kama yeye ni ukuta, tutajenga minara ya fedha juu yake. Na kama yeye ni mlango, tutamzungushia mbao za mierezi. [10] Mimi ni ukuta, nayo matiti yangu ni kama minara. Ndivyo ambavyo nimekuwa machoni pake kama yule anayeleta utoshelevu. [11] Solomoni alikuwa na shamba la mizabibu huko Baal-Hamoni; alikodisha shamba lake la mizabibu kwa wapangaji. Kila mmoja angeleta kwa ajili ya matunda yake shekeli 1,000 za fedha. [12] Lakini shamba langu la mizabibu ambalo ni langu mwenyewe ni langu kutoa; hizo shekeli 1,000 ni kwa ajili yako, ee Solomoni, na shekeli mia mbili ni kwa ajili ya wale wanaotunza matunda yake. [13] Wewe ukaaye bustanini pamoja na marafiki mliohudhuria, hebu nisikie sauti yako! [14] Njoo, mpenzi wangu, uwe kama swala au kama ayala kijana juu ya milima iliyojaa vikolezo.