[1] Nimekuja kwenye bustani yangu, dada yangu, bibi arusi wangu; nimekusanya manemane yangu pamoja na kikolezo changu. Nimekula sega langu la asali na asali yangu; nimekunywa divai yangu na maziwa yangu. Kuleni, enyi marafiki, mnywe; kunyweni ya kutosha, ee wapenzi. [2] Nililala lakini moyo wangu ulikuwa macho. Sikiliza! Mpenzi wangu anabisha: “Nifungulie, dada yangu, mpenzi wangu, hua wangu, asiye na hitilafu. Kichwa changu kimeloa umande, na nywele zangu manyunyu ya usiku.” [3] Nimevua joho langu: je, ni lazima nivae tena? Nimenawa miguu yangu: je, ni lazima niichafue tena? [4] Mpenzi wangu aliweka mkono wake kwenye tundu la komeo; moyo wangu ulianza kugonga kwa ajili yake. [5] Niliinuka kumfungulia mpenzi wangu, mikono yangu ikidondosha manemane, vidole vyangu vikitiririka manemane, penye vipini vya komeo. [6] Nilimfungulia mpenzi wangu, lakini mpenzi wangu alishaondoka; alikuwa amekwenda zake. Moyo wangu ulishuka kwa kuondoka kwake. Nilimtafuta lakini sikumpata. Nilimwita lakini hakunijibu. [7] Walinzi walinikuta walipokuwa wakifanya zamu za ulinzi mjini. Walinipiga, wakanijeruhi, wakaninyangʼanya joho langu, hao walinzi wa kuta! [8] Enyi binti za Yerusalemu, ninawaagiza: kama mkimpata mpenzi wangu, mtamwambia nini? Mwambieni ninazimia kwa mapenzi. [9] Je, mpendwa wako ni bora kuliko wengine namna gani, wewe uliye mzuri kupita wanawake wote? Je, mpendwa wako ni mzuri kuliko wengine, namna gani, hata unatuagiza hivyo? [10] Mpenzi wangu anangʼaa, tena ni mwekundu, wa kuvutia miongoni mwa wanaume kumi elfu. [11] Kichwa chake ni dhahabu safi kuliko zote, nywele zake ni za mawimbi na ni nyeusi kama kunguru. [12] Macho yake ni kama ya hua kandokando ya vijito vya maji, aliyeogeshwa kwenye maziwa, yaliyopangwa kama vito vya thamani. [13] Mashavu yake ni kama matuta ya vikolezo yakitoa manukato. Midomo yake ni kama yungiyungi inayodondosha manemane. [14] Mikono yake ni fimbo za dhahabu iliyopambwa kwa krisolitho. Mwili wake ni kama pembe ya ndovu iliyongʼarishwa iliyopambwa na yakuti samawi. [15] Miguu yake ni nguzo za marmar zilizosimikwa katika vitako vya dhahabu safi. Sura yake ni kama Lebanoni, bora kama miti yake ya mierezi. [16] Kinywa chake chenyewe ni utamu, kwa ujumla yeye ni wa kupendeza. Huyu ndiye mpenzi wangu, huyu ndiye rafiki yangu, ee binti za Yerusalemu.