[1] Hekima amejenga nyumba yake; amechonga nguzo zake saba. [2] Ameandaa nyama na kuchanganya divai yake; pia ameandaa meza yake. [3] Amewatuma watumishi wake wa kike, naye huita kutoka mahali pa juu sana pa mji. [4] Anawaambia wale wasio na akili, “Wote ambao ni wajinga na waje hapa! [5] Njooni, mle chakula changu na mnywe divai niliyoichanganya. [6] Acheni njia zenu za ujinga nanyi mtaishi; tembeeni katika njia ya ufahamu. [7] “Yeyote anayemkosoa mwenye mzaha hukaribisha matukano; yeyote anayekemea mtu mwovu hupatwa na matusi. [8] Usimkemee mwenye mzaha la sivyo atakuchukia; mkemee mwenye hekima naye atakupenda. [9] Mfundishe mtu mwenye hekima naye atakuwa na hekima zaidi; mfundishe mtu mwadilifu naye atazidi kufundishika. [10] “Kumcha BWANA ndicho chanzo cha hekima, na kumjua Aliye Mtakatifu ni ufahamu. [11] Kwa maana kwa msaada wangu siku zako zitakuwa nyingi, na miaka itaongezwa katika maisha yako. [12] Kama wewe una hekima, hekima yako itakupa tuzo; kama wewe ni mtu wa mzaha, wewe mwenyewe ndiwe utateseka.” [13] Mwanamke aitwaye Mpumbavu ana kelele; hana adabu na hana maarifa. [14] Huketi kwenye mlango wa nyumba yake, juu ya kiti katika mahali pa juu sana pa mji, [15] akiita wale wapitao karibu, waendao moja kwa moja kwenye njia yao. [16] Anawaambia wale wasio na akili, “Wote ambao ni wajinga na waje hapa ndani!” [17] “Maji yaliyoibiwa ni matamu; chakula kinacholiwa sirini ni kitamu!” [18] Lakini hawajui hata kidogo kuwa wafu wako humo, kwamba wageni wake huyo mwanamke wako katika vilindi vya kuzimu.