Mithali 10:1-32 ONEN
[1] Mithali za Solomoni: Mwana mwenye hekima huleta furaha kwa baba yake, lakini mwana mpumbavu huleta huzuni kwa mama yake. [2] Hazina zilizopatikana kwa njia mbaya hazifai, lakini uadilifu huokoa kutoka mautini. [3] BWANA hawaachi waadilifu kukaa njaa, lakini hupinga tamaa ya mtu mwovu. [4] Mikono mivivu hufanya mtu kuwa maskini lakini mikono yenye bidii huleta utajiri. [5] Yeye akusanyaye mazao wakati wa kiangazi ni mwana mwenye hekima, lakini yeye alalaye wakati wa mavuno ni mwana mwenye kuaibisha. [6] Baraka huwa taji kichwani mwa mwenye haki, lakini jeuri hufunika kinywa cha mwovu. [7] Kumbukumbu ya mwenye haki itakuwa baraka, lakini jina la mwovu litaoza. [8] Mwenye hekima moyoni hupokea maagizo, lakini mpumbavu apayukaye huangamia. [9] Mtu mwadilifu hutembea salama, lakini mtu aendaye katika njia zilizopotoka atagunduliwa. [10] Yeye akonyezaye kwa nia mbaya husababisha huzuni, naye mpumbavu apayukaye huangamia. [11] Kinywa cha mwenye haki ni chemchemi ya uzima, lakini jeuri hufunika kinywa cha mwovu. [12] Chuki huchochea faraka, lakini upendo husitiri mabaya yote. [13] Hekima hupatikana katika midomo ya wenye kupambanua, lakini fimbo ni kwa ajili ya mgongo wake asiye na ufahamu. [14] Wenye hekima huhifadhi maarifa, bali kinywa cha mpumbavu hualika maangamizi. [15] Mali ya tajiri ni mji wake wenye ngome, bali ufukara ni maangamizi ya maskini. [16] Ujira wa wenye haki huwaletea uzima, lakini mapato ya waovu huwaletea adhabu. [17] Anayekubali kuadibishwa yuko katika njia ya uzima, lakini yeyote anayepuuza maonyo hupotosha wengine. [18] Yeye afichaye chuki yake ana midomo ya uongo, na yeyote anayeeneza uchonganishi ni mpumbavu. [19] Wakati maneno ni mengi, dhambi haikosekani, lakini yeye ambaye huzuia ulimi wake ni mwenye busara. [20] Ulimi wa mwenye haki ni fedha iliyo bora, bali moyo wa mwovu una thamani ndogo. [21] Midomo ya mwenye haki hulisha wengi, lakini wapumbavu hufa kwa kukosa ufahamu. [22] Baraka ya BWANA hutajirisha, wala haichanganyi huzuni. [23] Mpumbavu hufurahia tabia mbaya, lakini mtu mwenye ufahamu hupendezwa na hekima. [24] Kile anachoogopa mwovu ndicho kitakachompata; kile anachoonea shauku mwenye haki atapewa. [25] Tufani inapopita, waovu hutoweka, lakini wenye haki husimama imara milele. [26] Kama siki ilivyo kwa meno na moshi kwa macho, ndivyo alivyo mvivu kwa wale waliomtuma. [27] Kumcha BWANA huongeza urefu wa maisha, lakini miaka ya mwovu inafupishwa. [28] Tarajio la mwenye haki ni furaha, bali matumaini ya mwovu huwa si kitu. [29] Njia ya BWANA ni kimbilio kwa wenye haki, lakini ni maangamizi ya wale watendao mabaya. [30] Kamwe wenye haki hawataondolewa, bali waovu hawatasalia katika nchi. [31] Kinywa cha mwenye haki hutoa hekima, bali ulimi wa upotovu utakatwa. [32] Midomo ya wenye haki inajua kile kinachofaa, bali kinywa cha mwovu hujua kile kilichopotoka tu.
