Mithali 8:1-36 ONEN
[1] Je, hekima haitani? Je, ufahamu hapazi sauti? [2] Juu ya miinuko karibu na njia, penye njia panda, ndipo asimamapo; [3] kando ya malango yaelekeayo mjini, kwenye maingilio, hulia kwa sauti kubwa, akisema: [4] “Ni ninyi wanaume, ninaowaita; ninapaza sauti yangu kwa wanadamu wote. [5] Ninyi ambao ni wajinga, pateni akili; ninyi mlio wapumbavu, pateni ufahamu. [6] Sikilizeni, kwa maana nina mambo muhimu ya kusema; ninafungua midomo yangu kusema lililo sawa. [7] Kinywa changu husema lililo kweli, kwa maana midomo yangu huchukia uovu. [8] Maneno yote ya kinywa changu ni haki; hakuna mojawapo lililopotoka wala ukaidi. [9] Kwa wenye kupambanua yote ni sahihi; hayana kasoro kwa wale wenye maarifa. [10] Chagua mafundisho yangu badala ya fedha, maarifa badala ya dhahabu safi, [11] kwa maana hekima ina thamani kuliko marijani na hakuna chochote unachohitaji kinacholingana naye. [12] “Mimi hekima, nakaa pamoja na busara; ninamiliki maarifa na busara. [13] Kumcha BWANA ni kuchukia uovu; ninachukia kiburi na majivuno, tabia mbaya na mazungumzo potovu. [14] Ushauri na hukumu sahihi ni vyangu; nina ufahamu na nina nguvu. [15] Kwa msaada wangu wafalme hutawala na watawala hutunga sheria zilizo za haki, [16] kwa msaada wangu wakuu hutawala, na wenye vyeo wote watawalao dunia. [17] Nawapenda wale wanipendao, na wale wanitafutao kwa bidii wataniona. [18] Utajiri na heshima viko kwangu, utajiri udumuo na mafanikio. [19] Tunda langu ni bora kuliko dhahabu safi; kile nitoacho hupita fedha iliyo bora. [20] Natembea katika njia ya unyofu katika mapito ya haki, [21] nawapa utajiri wale wanipendao na kuzijaza hazina zao. [22] “BWANA aliniumba mwanzoni mwa kazi yake, kabla ya matendo yake ya zamani; [23] niliteuliwa tangu milele, tangu mwanzoni, kabla ya dunia kuumbwa. [24] Wakati hazijakuwepo bahari, nilikwishazaliwa, wakati hazijakuwepo chemchemi zilizojaa maji; [25] kabla milima haijawekwa mahali pake, kabla vilima havijakuwepo, nilikwishazaliwa, [26] kabla hajaumba dunia wala mashamba yake au vumbi lolote la dunia. [27] Nilikuwepo alipoziweka mbingu mahali pake, wakati alichora mstari wa upeo wa macho juu ya uso wa kilindi, [28] wakati aliweka mawingu juu na kuziweka imara chemchemi za bahari, [29] wakati aliiwekea bahari mpaka wake ili maji yasivunje agizo lake, na wakati aliweka misingi ya dunia. [30] Wakati huo nilikuwa fundi stadi kando yake. Nilijazwa na furaha siku baada ya siku, nikifurahi daima mbele zake, [31] nikifurahi katika dunia yake yote nami nikiwafurahia wanadamu. [32] “Basi sasa wanangu, nisikilizeni; heri wale wanaozishika njia zangu. [33] Sikilizeni mafundisho yangu mwe na hekima; msiyapuuze. [34] Heri mtu yule anisikilizaye mimi, akisubiri siku zote malangoni mwangu, akingoja kwenye vizingiti vya mlango wangu. [35] Kwa maana yeyote anipataye mimi amepata uzima na kujipatia kibali kutoka kwa BWANA. [36] Lakini yeyote ashindwaye kunipata hujiumiza mwenyewe; na wote wanichukiao mimi hupenda mauti.”
