[1] Mwanangu, shika maneno yangu na kuzihifadhi amri zangu ndani yako. [2] Shika amri zangu nawe utaishi; linda mafundisho yangu kama mboni ya jicho lako. [3] Yafunge katika vidole vyako; yaandike katika kibao cha moyo wako. [4] Mwambie hekima, “Wewe ni dada yangu,” uite ufahamu jamaa yako; [5] watakuepusha na mwanamke mzinzi, kutokana na mwanamke mpotovu na maneno yake ya kubembeleza. [6] Kwenye dirisha la nyumba yangu nilitazama nje kupitia upenyo kwenye mwimo wa dirisha. [7] Niliona miongoni mwa wajinga, nikagundua miongoni mwa wanaume vijana, kijana asiye na akili. [8] Alikuwa akishuka njiani karibu na pembe ya kwake, akielekea kwenye nyumba ya huyo mwanamke [9] wakati wa machweo, jua likipungua nuru yake, giza la usiku lilipokuwa likiingia. [10] Ndipo huyo mwanamke akatoka kumlaki, hali amevaa kama kahaba akiwa na nia ya udanganyifu. [11] (Ni mwanamke mwenye makelele na mkaidi, miguu yake haitulii nyumbani; [12] mara kwenye barabara za mji, mara kwenye viwanja vikubwa, kwenye kila pembe huvizia.) [13] Huyo mwanamke alimkumbatia kijana na kumbusu, na kwa uso usio na haya akamwambia: [14] “Nina sadaka za amani nyumbani; leo nimetimiza nadhiri zangu. [15] Kwa hiyo nimetoka nje kukulaki; nimekutafuta na nimekupata! [16] Nimetandika kitanda changu kwa kitani za rangi kutoka Misri. [17] Nimetia manukato kitanda changu kwa manemane, udi na mdalasini. [18] Njoo, tuzame katika mapenzi mpaka asubuhi; tujifurahishe wenyewe kwa mapenzi! [19] Mume wangu hayupo nyumbani; amekwenda safari ya mbali. [20] Amechukua mkoba uliojazwa fedha na hatakuwepo nyumbani karibuni.” [21] Kwa maneno laini yule mwanamke akampotosha; alimshawishi kwa maneno yake laini. [22] Mara huyo kijana alimfuata yule mwanamke kama fahali aendaye machinjoni, kama kulungu aingiaye kwenye kitanzi, [23] mpaka mshale umchome ini lake, kama ndege anayenaswa kwenye mtego, bila kujua itamgharimu maisha yake. [24] Sasa basi wanangu, nisikilizeni; sikilizeni kwa makini nisemalo. [25] Usiruhusu moyo wako ugeukie njia za huyo mwanamke, wala usitangetange katika mapito yake. [26] Aliowaangusha ni wengi; aliowachinja ni kundi kubwa. [27] Nyumba yake ni njia kuu iendayo kaburini, ielekeayo chini kwenye vyumba vya mauti.