Mithali 6:1-35 ONEN
[1] Mwanangu, kama umekuwa mdhamini wa jirani yako, ikiwa umeshika mikono kwa kuweka ahadi kwa ajili ya mwingine, [2] kama umetegwa na ulichosema, umenaswa kwa maneno ya kinywa chako, [3] basi fanya hivi mwanangu, ili ujiweke huru, kwa kuwa umeanguka mikononi mwa jirani yako: Nenda ukajinyenyekeshe kwake; msihi jirani yako! [4] Usiruhusu usingizi machoni pako, usiruhusu kope zako zisinzie. [5] Jiweke huru, kama swala mkononi mwa mwindaji, kama ndege kutoka kwenye mtego wa mwindaji. [6] Ewe mvivu, mwendee mchwa; zitafakari njia zake ukapate hekima! [7] Kwa maana yeye hana msimamizi, wala mwangalizi, au mtawala, [8] lakini hujiwekea akiba wakati wa kiangazi na hukusanya chakula chake wakati wa mavuno. [9] Ewe mvivu, utalala hata lini? Utaamka lini kutoka usingizi wako? [10] Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, bado kukunja mikono kidogo upate kupumzika: [11] hivyo umaskini utakuja juu yako kama mnyangʼanyi, na kupungukiwa kutakujia kama mtu mwenye silaha. [12] Mtu mbaya sana na mlaghai, ambaye huzungukazunguka na maneno ya upotovu, [13] ambaye anakonyeza kwa jicho lake, anayetoa ishara kwa miguu yake na kuashiria kwa vidole vyake, [14] ambaye hupanga ubaya kwa udanganyifu moyoni mwake: daima huchochea fitina. [15] Kwa hiyo maafa yatamkumba ghafula; ataangamizwa mara, pasipo msaada. [16] Kuna vitu sita anavyovichukia BWANA, naam, viko saba vilivyo chukizo kwake: [17] macho ya kiburi, ulimi udanganyao, mikono imwagayo damu isiyo na hatia, [18] moyo uwazao mipango miovu, miguu iliyo myepesi kukimbilia uovu, [19] shahidi wa uongo ambaye humwaga uongo, na mtu ambaye huchochea fitina kati ya ndugu. [20] Mwanangu, zishike amri za baba yako, wala usiyaache mafundisho ya mama yako. [21] Yafunge katika moyo wako daima, yakaze kuizunguka shingo yako. [22] Wakati utembeapo, yatakuongoza; wakati ulalapo, yatakulinda; wakati uamkapo, yatazungumza nawe. [23] Kwa maana amri hizi ni taa, mafundisho haya ni mwanga na maonyo ya maadili ni njia ya uzima, [24] yakikulinda na mwanamke aliyepotoka, kutokana na maneno laini ya mwanamke aliyepotoka. [25] Moyo wako usitamani uzuri wake wala macho yake yasikuteke, [26] kwa maana kahaba atakufanya uwe maskini, hata ukose kipande cha mkate, naye mwanamke mzinzi huwinda maisha yako hasa. [27] Je, mtu aweza kuchotea moto kwenye paja lake bila nguo zake kuungua? [28] Je, mtu aweza kutembea juu ya makaa ya moto yanayowaka bila miguu yake kuungua? [29] Ndivyo alivyo mtu alalaye na mke wa mwanaume mwingine; hakuna yeyote amgusaye huyo mwanamke ambaye hataadhibiwa. [30] Watu hawamdharau mwizi kama akiiba kukidhi njaa yake wakati ana njaa. [31] Pamoja na hayo, kama akikamatwa, lazima alipe mara saba, ingawa inamgharimu utajiri wote wa nyumba yake. [32] Lakini mwanaume aziniye na mwanamke hana akili kabisa; yeyote afanyaye hivyo hujiangamiza mwenyewe. [33] Mapigo na aibu ni fungu lake na aibu yake haitafutika kamwe; [34] kwa maana wivu huamsha ghadhabu ya mume, naye hataonyesha huruma alipizapo kisasi. [35] Hatakubali fidia yoyote; atakataa malipo, hata yakiwa makubwa kiasi gani.
