[1] Mwanangu, sikiliza kwa makini hekima yangu, sikiliza vizuri maneno yangu ya busara, [2] ili uweze kutunza busara na midomo yako ihifadhi maarifa. [3] Kwa maana midomo ya mwanamke kahaba hudondoza asali, na maneno ya kinywa chake ni laini kuliko mafuta; [4] lakini mwisho wake ni mchungu kama nyongo, mkali kama upanga ukatao kuwili. [5] Miguu yake hushuka kuelekea kwenye kifo; hatua zake huelekea moja kwa moja kaburini. [6] Yeye hafikiri juu ya njia ya uzima; njia zake zimepotoka, lakini yeye hajui. [7] Sasa basi wanangu, nisikilizeni; msiache ninalowaambia. [8] Njia zenu ziwe mbali naye, msiende karibu na mlango wa nyumba yake, [9] usije ukatoa nguvu zako nzuri kwa wengine na miaka yako kwa aliye mkatili, [10] wageni wasije wakasherehekea utajiri wako na jitihada yako ikatajirisha nyumba ya mwanaume mwingine. [11] Mwishoni mwa maisha yako utalia kwa uchungu, wakati nyama na mwili wako vimechakaa. [12] Utasema, “Tazama jinsi gani nilivyochukia adhabu! Tazama jinsi moyo wangu ulivyodharau maonyo! [13] Sikuwatii walimu wangu wala kuwasikiliza wakufunzi wangu. [14] Nimefika ukingoni mwa maangamizi kabisa katikati ya kusanyiko lote.” [15] Kunywa maji kutoka kwenye kisima chako mwenyewe, maji yanayotiririka kutoka kwenye kisima chako mwenyewe. [16] Je, chemchemi zako zifurike katika barabara za mji na vijito vyako vya maji viwanjani? [17] Na viwe vyako mwenyewe, kamwe visishirikishwe wageni. [18] Chemchemi yako na ibarikiwe na umfurahie mke wa ujana wako. [19] Kulungu jike apendaye, kulungu mzuri: matiti yake na yakutosheleze siku zote, nawe utekwe daima na upendo wake. [20] Kwa nini mwanangu, utekwe na mwanamke kahaba? Kwa nini ukumbatie kifua cha mke wa mwanaume mwingine? [21] Kwa maana njia za mtu ni wazi kabisa mbele za BWANA, naye huyapima mapito yake yote. [22] Matendo mabaya ya mtu mwovu humnasa yeye mwenyewe; kamba za dhambi yake humkamata kwa nguvu. [23] Atakufa kwa kukosa nidhamu, akipotoshwa kwa upumbavu wake mwenyewe.