[1] Sikilizeni wanangu, mafundisho ya baba yenu; sikilizeni kwa makini na mpate ufahamu. [2] Ninawapa mafundisho ya maana, kwa hiyo msiyaache mafundisho yangu. [3] Nilipokuwa mvulana mdogo katika nyumba ya baba yangu, ningali mchanga na mtoto pekee kwa mama yangu, [4] baba alinifundisha akisema, “Yashike maneno yangu yote kwa moyo wako wote; yashike maagizo yangu na wewe utaishi. [5] Pata hekima, pata ufahamu; usiyasahau maneno yangu wala usiyaache. [6] Usimwache hekima naye atakuweka salama; mpende, naye atakulinda. [7] Hekima ni bora kuliko vitu vyote; kwa hiyo jipe hekima. Hata ikikugharimu vyote ulivyo navyo, pata ufahamu. [8] Mstahi, naye atakukweza; mkumbatie, naye atakuheshimu. [9] Atakuvika shada la neema kichwani mwako na kukupa taji ya utukufu.” [10] Sikiliza mwanangu, kubali ninachokuambia, nayo miaka ya maisha yako itakuwa mingi. [11] Ninakuongoza katika njia ya hekima na kukuongoza katika mapito yaliyonyooka. [12] Utembeapo, hatua zako hazitazuiliwa; ukimbiapo, hutajikwaa. [13] Mkamate sana elimu, usimwache aende zake; mshike, maana yeye ni uzima wako. [14] Usiuweke mguu wako katika njia ya waovu wala usitembee katika njia ya watu wabaya. [15] Epukana nayo, usisafiri katika njia hiyo; achana nayo, na uelekee njia yako. [16] Kwa kuwa hawawezi kulala mpaka watende uovu; wanashindwa hata kusinzia mpaka wamwangushe mtu. [17] Wanakula mkate wa uovu, na kunywa mvinyo wa jeuri. [18] Njia ya wenye haki ni kama nuru ya kwanza ya mapambazuko, ambayo hungʼaa zaidi na zaidi mpaka mchana mkamilifu. [19] Lakini njia ya waovu ni kama giza nene; hawajui kinachowafanya wajikwae. [20] Mwanangu, yasikilize kwa makini yale ninayokuambia; sikiliza kwa makini maneno yangu. [21] Usiruhusu yaondoke machoni pako, yahifadhi ndani ya moyo wako; [22] kwa sababu ni uzima kwa wale wanaoyapata na afya kwa mwili wote wa mwanadamu. [23] Zaidi ya yote, linda moyo wako, kuliko yote uyalindayo, maana ndiko zitokako chemchemi za uzima. [24] Epusha kinywa chako na ukaidi; weka mazungumzo machafu mbali na midomo yako. [25] Macho yako na yatazame mbele, kaza macho yako moja kwa moja mbele yako. [26] Sawazisha mapito ya miguu yako na njia zako zote ziwe zimethibitika. [27] Usigeuke kulia wala kushoto; epusha mguu wako na ubaya.