Mithali 3:1-35 ONEN
[1] Mwanangu, usisahau mafundisho yangu, bali zitunze amri zangu moyoni mwako, [2] kwa kuwa zitakuongezea miaka mingi ya maisha yako na kukuletea mafanikio. [3] Usiache kamwe upendo na uaminifu vitengane nawe; vifunge shingoni mwako, viandike katika ubao wa moyo wako. [4] Ndipo utapata kibali na jina zuri mbele za Mungu na mwanadamu. [5] Mtumaini BWANA kwa moyo wako wote wala usizitegemee akili zako mwenyewe; [6] katika njia zako zote mkiri yeye, naye atayanyoosha mapito yako. [7] Usiwe mwenye hekima machoni pako mwenyewe; mche BWANA ukajiepushe na uovu. [8] Hii itakuletea afya mwilini mwako, na mafuta kwenye mifupa yako. [9] Mheshimu BWANA kwa mali zako na kwa malimbuko ya mazao yako yote; [10] ndipo ghala zako zitakapojaa hadi kufurika, viriba vyako vitafurika kwa mvinyo mpya. [11] Mwanangu, usiidharau adhabu ya BWANA na usichukie kukaripiwa naye, [12] kwa sababu BWANA huwaadibisha wale awapendao, kama vile baba afanyavyo kwa mwana apendezwaye naye. [13] Heri mtu yule aonaye hekima, mtu yule apataye ufahamu, [14] kwa maana hekima ana faida kuliko fedha na mapato yake ni bora kuliko ya dhahabu safi. [15] Hekima ana thamani kuliko marijani; hakuna chochote unachokitamani kinachoweza kulinganishwa naye. [16] Maisha marefu yako katika mkono wake wa kuume; katika mkono wake wa kushoto kuna utajiri na heshima. [17] Njia zake zinapendeza, mapito yake yote ni amani. [18] Yeye ni mti wa uzima kwa wale wanaomkumbatia; wale wamshikao watabarikiwa. [19] Kwa hekima BWANA aliiweka misingi ya dunia, kwa ufahamu aliziweka mbingu mahali pake; [20] kwa maarifa yake vilindi viligawanywa, nayo mawingu yanadondosha umande. [21] Mwanangu, hifadhi maamuzi mema na busara, usiache vitoke machoni pako; [22] ndipo vitakapokuwa uzima nafsini mwako na pambo la neema shingoni mwako. [23] Kisha utaenda katika njia yako salama, wala mguu wako hautajikwaa; [24] ulalapo, hautaogopa; ulalapo usingizi wako utakuwa mtamu. [25] Usiogope maafa ya ghafula au maangamizi yanayowapata waovu, [26] kwa kuwa BWANA atakuwa tumaini lako na kuepusha mguu wako kunaswa katika mtego. [27] Usizuie wema kwa wale wanaostahili ikiwa katika uwezo wako kutenda. [28] Usimwambie jirani yako, “Njoo baadaye, nitakupa kesho”: wakati wewe unacho kitu kile karibu nawe. [29] Usifanye hila ya kumdhuru jirani yako, ambaye anaishi karibu na wewe akikuamini. [30] Usimshtaki mtu bila sababu, wakati hajakutenda dhara lolote. [31] Usimwonee wivu mtu mwenye jeuri wala kuchagua njia yake iwayo yote, [32] kwa kuwa BWANA humchukia mtu mpotovu, lakini siri yake iko kwa mwenye haki. [33] Laana ya BWANA i juu ya nyumba ya mwovu, lakini yeye huibariki nyumba ya mwenye haki. [34] Huwadhihaki wale wanaodhihaki, lakini huwapa neema wale wanyenyekevu. [35] Wenye hekima hurithi heshima, bali huwaaibisha wapumbavu.
