[1] Mwanangu, kama utayakubali maneno yangu na kuyaweka akiba maagizo yangu ndani mwako, [2] kutega sikio lako kwenye hekima na kuweka moyo wako katika ufahamu, [3] na kama ukiita busara na kuita kwa sauti ufahamu, [4] na kama utaitafuta kama fedha na kuitafuta sana kama hazina iliyofichwa, [5] ndipo utakapoelewa kumcha BWANA na kupata maarifa ya Mungu. [6] Kwa maana BWANA hutoa hekima, na kinywani mwake hutoka maarifa na ufahamu. [7] Anahifadhi ushindi kwa ajili ya mwadilifu, yeye ni ngao kwa wale wasio na lawama, [8] kwa kuwa hulinda mwenendo wa mwenye haki na kuhifadhi njia ya waaminifu wake. [9] Ndipo utafahamu lipi lililo kweli na haki na sawa: yaani kila njia nzuri. [10] Kwa maana hekima itaingia moyoni mwako, nayo maarifa yataifurahisha nafsi yako. [11] Busara itakuhifadhi na ufahamu utakulinda. [12] Hekima itakuokoa kutoka njia za waovu, kutoka kwa watu ambao maneno yao yamepotoka, [13] wale waachao mapito yaliyonyooka wakatembea katika njia za giza, [14] wale wapendao kutenda mabaya na kufurahia upotovu wa ubaya, [15] ambao mapito yao yamepotoka na ambao ni wapotovu katika njia zao. [16] Itakuokoa pia kutokana na mwanamke kahaba, kutokana na mke aliyepotoka mwenye maneno ya kushawishi kutenda ubaya, [17] aliyemwacha mwenzi wa ujana wake na kupuuza agano alilofanya mbele ya Mungu. [18] Kwa maana nyumba yake huelekea kwenye kifo na mapito yake kwenye roho za waliokufa. [19] Hakuna yeyote aendaye kwake akarudi, au kufikia mapito ya uzima. [20] Hivyo utatembea katika njia za watu wema na kushikamana na mapito ya wenye haki. [21] Kwa maana wanyofu wataishi katika nchi, nao wasio na lawama watabakia ndani yake. [22] Bali waovu watakatiliwa mbali kutoka nchi, nao wasio waaminifu watangʼolewa kutoka humo.