Mithali 28:1-28 ONEN
[1] Mtu mwovu hukimbia ingawa hakuna yeyote anayemfukuza, bali wenye haki ni wajasiri kama simba. [2] Wakati nchi inapokuwa na uasi, inakuwa na viongozi wengi, bali mwenye ufahamu na maarifa hudumisha utaratibu. [3] Mtu maskini amwoneaye yeye aliye maskini zaidi ni kama mvua ya dhoruba isiyosaza mazao. [4] Wale waiachao sheria huwasifu waovu, bali wale waishikao sheria huwapinga. [5] Watu wabaya hawaelewi haki, bali wale wamtafutao BWANA wanaielewa kikamilifu. [6] Afadhali maskini ambaye mwenendo wake hauna lawama kuliko tajiri ambaye njia zake ni potovu. [7] Yeye ashikaye sheria ni mwana mwenye ufahamu, bali rafiki wa walafi humwaibisha baba yake. [8] Yeye aongezaye utajiri wake kwa riba kubwa mno hukusanya kwa ajili ya mwingine, ambaye atawahurumia maskini. [9] Kama mtu yeyote akikataa kusikia sheria, hata maombi yake ni chukizo. [10] Yeye ambaye humwongoza mwenye haki kwenye mapito mabaya, ataanguka kwenye mtego wake mwenyewe, bali wasio na lawama watapokea urithi mwema. [11] Mtu tajiri anaweza kuwa na hekima machoni pake mwenyewe, bali mtu maskini mwenye ufahamu atamfichua. [12] Mwenye haki ashindapo, kuna furaha kubwa, bali waovu watawalapo, watu hujificha. [13] Yeye afichaye dhambi zake hatafanikiwa, bali yeyote aziungamaye na kuziacha hupata rehema. [14] Amebarikiwa mtu ambaye siku zote humcha BWANA, bali yeye afanyaye moyo wake kuwa mgumu huangukia kwenye taabu. [15] Kama simba angurumaye au dubu ashambuliaye, ndivyo alivyo mtu mwovu atawalaye wanyonge. [16] Mtawala dhalimu hana akili, bali yeye achukiaye mapato ya udhalimu atafurahia maisha marefu. [17] Mtu mwenye kusumbuliwa na hatia ya kuua atakuwa mtoro mpaka kufa; mtu yeyote na asimsaidie. [18] Yeye ambaye mwenendo wake hauna lawama hulindwa salama, bali yeye ambaye njia zake ni potovu ataanguka ghafula. [19] Yeye alimaye shamba lake atakuwa na chakula tele, bali yule afuataye mambo ya upuzi atakuwa na umaskini wa kumtosha. [20] Mtu mwaminifu atabarikiwa sana, bali yeye atamaniye kupata utajiri kwa haraka hataacha kuadhibiwa. [21] Kuonyesha upendeleo si vizuri, hata hivyo mtu atafanya kosa kwa kipande cha mkate. [22] Mtu mchoyo ana tamaa ya kupata utajiri, naye hana habari kuwa umaskini unamngojea. [23] Yeye amkemeaye mtu mwishoni hupata kibali zaidi, kuliko mwenye maneno ya kusifu isivyostahili. [24] Yeye amwibiaye babaye au mamaye na kusema, “Si kosa,” yeye ni mwenzi wa yule aharibuye. [25] Mtu mwenye tamaa huchochea fitina, bali yule amtegemeaye BWANA atafanikiwa. [26] Yeye ajitumainiaye mwenyewe ni mpumbavu, bali yeye atembeaye katika hekima hulindwa salama. [27] Yeye ampaye maskini hatapungukiwa na kitu chochote, bali yeye awafumbiaye maskini macho hupata laana nyingi. [28] Wakati waovu watawalapo, watu huenda mafichoni, bali waovu wanapoangamia, wenye haki hufanikiwa.
