[1] Mtu anayeendelea kuwa na shingo ngumu baada ya maonyo mengi, ataangamia ghafula, wala hapati dawa. [2] Wenye haki wanapostawi, watu hufurahi; waovu watawalapo, watu hulia kwa huzuni. [3] Mtu apendaye hekima huleta furaha kwa baba yake, bali aambatanaye na makahaba hutapanya mali yake. [4] Kwa haki mfalme huipa nchi uthabiti, bali mfalme aliye na tamaa ya rushwa huiangamiza. [5] Yeyote amsifuye jirani yake isivyostahili, anautandaza wavu kuitega miguu yake. [6] Mtu mbaya hutegwa na dhambi yake mwenyewe bali mwenye haki huweza kuimba na kufurahi. [7] Mwenye haki hujali haki kwa ajili ya maskini, bali mwovu hajishughulishi na hilo. [8] Wenye mzaha huuchochea mji, bali watu wenye hekima hugeuzia mbali hasira. [9] Kama mwenye hekima akienda mahakamani na mpumbavu, mpumbavu hukasirika na kudhihaki, wala hakuna amani. [10] Watu wamwagao damu humchukia mtu mwadilifu na hutafuta kumuua mtu mnyofu. [11] Mpumbavu huonyesha hasira yake yote, bali mwenye hekima hujizuia. [12] Kama mtawala akisikiliza uongo, maafisa wake wote huwa waovu. [13] Mtu maskini na mtu anayeonea wanafanana kwa jambo hili: BWANA hutia nuru macho yao wote wawili. [14] Kama mfalme akiwaamua maskini kwa haki, kiti chake cha enzi kitakuwa thabiti siku zote. [15] Fimbo ya maonyo hutia hekima, bali mtoto aliyeachiwa bila maonyo humwaibisha mama yake. [16] Wakati waovu wanapostawi, pia dhambi vivyo hivyo, lakini wenye haki wataliona anguko lao. [17] Mrudi mwanao, naye atakupa amani, atakufurahisha nafsi yako. [18] Mahali pasipo na ufunuo, watu kujizuia, bali ana heri mtu yule aishikaye sheria. [19] Mtumishi hawezi kuonywa kwa maneno matupu, ajapoelewa, hataitikia. [20] Je, unamwona mtu azungumzaye kwa haraka? Kuna matumaini zaidi kwa mpumbavu kuliko yeye. [21] Kama mtu akimdekeza mtumishi wake tangu ujanani, atamletea sikitiko mwishoni. [22] Mtu mwenye hasira huchochea ugomvi, naye mtu mwenye hasira ya haraka hutenda dhambi nyingi. [23] Kiburi cha mtu humshusha, bali mtu mwenye roho ya unyenyekevu hupata heshima. [24] Anayekubaliana na mwizi ni adui wa nafsi yake mwenyewe; huapishwa lakini hathubutu kushuhudia. [25] Kuwaogopa watu huwa ni mtego, bali yeyote amtumainiaye BWANA atakuwa salama. [26] Wengi hutafuta kusikilizwa na mtawala, bali mtu hupata haki kutoka kwa BWANA. [27] Mwenye haki huwachukia sana wasio waaminifu; waovu huwachukia sana wenye haki.