Mithali 27:1-27 ONEN
[1] Usijisifu kwa ajili ya kesho, kwa kuwa hujui ni nini kitakachozaliwa kwa siku moja. [2] Mwache mwingine akusifu, wala si kinywa chako mwenyewe; mtu mwingine afanye hivyo na si midomo yako mwenyewe. [3] Jiwe ni zito na mchanga ni mzigo, lakini kukasirishwa na mpumbavu ni kuzito kuliko vyote viwili. [4] Hasira ni ukatili na ghadhabu kali ni gharika, lakini ni nani awezaye kusimama mbele ya wivu? [5] Afadhali karipio la wazi kuliko upendo uliofichika. [6] Majeraha kutoka kwa rafiki yaonyesha uaminifu, bali kubusu kwa adui ni kwingi sana. [7] Yeye aliyeshiba huchukia kabisa asali, bali kwa mwenye njaa hata kile kilicho kichungu kwake ni kitamu. [8] Kama ndege atangatangavyo mbali na kiota chake, ndivyo alivyo mtu atangatangaye mbali na nyumbani mwake. [9] Manukato na uvumba huleta furaha moyoni, nao uzuri wa rafiki huchipuka kutoka kwenye ushauri wake wa uaminifu. [10] Usimwache rafiki yako wala rafiki wa baba yako, tena usiende nyumbani mwa ndugu yako wakati umepatwa na maafa. Bora jirani wa karibu kuliko ndugu aliye mbali. [11] Mwanangu, uwe na hekima, nawe ulete furaha moyoni mwangu, ndipo nitakapoweza kumjibu yeyote anitendaye kwa dharau. [12] Mtu mwenye busara huona hatari na kujificha, bali mjinga huendelea mbele nayo ikamtesa. [13] Chukua vazi la yule awekaye dhamana kwa ajili ya mgeni; lishikilie iwe dhamana kama anafanya hivyo kwa ajili ya mwanamke mpotovu. [14] Kama mtu akimbariki jirani yake kwa sauti kuu asubuhi na mapema, itahesabiwa kama ni laana. [15] Mke mgomvi ni kama matone yasiyokoma ya siku ya mvua. [16] Kumzuia yeye ni kama kuuzuia upepo au kukamata mafuta kwa kiganja cha mkono. [17] Kama vile chuma kinoavyo chuma, ndivyo mtu amnoavyo mwenzake. [18] Yeye autunzaye mtini atakula tunda lake, naye amtunzaye bwana wake ataheshimiwa. [19] Kama uso uonekanavyo kwenye maji, ndivyo hivyo moyo wa mtu humwonyesha alivyo. [20] Kuzimu na Uharibifu havishibi kadhalika macho ya mwanadamu. [21] Kalibu ni kwa ajili ya fedha na tanuru kwa ajili ya dhahabu, bali mtu hupimwa kwa sifa azipokeazo. [22] Hata ukimtwanga mpumbavu kwenye kinu, ukimtwanga kama nafaka kwa mchi, hutauondoa upumbavu wake. [23] Hakikisha kuwa unajua hali ya makundi yako ya kondoo na mbuzi, angalia kwa bidii ngʼombe zako. [24] Kwa kuwa utajiri haudumu milele, nayo taji haidumu vizazi vyote. [25] Wakati majani makavu yameondolewa na mapya yamechipua, nayo majani toka milimani yamekusanywa, [26] wana-kondoo watakupatia mavazi na mbuzi thamani ya shamba. [27] Utakuwa na maziwa mengi ya mbuzi kukulisha wewe na jamaa yako, na kuwalisha watumishi wako wa kike.
