Mithali 26:1-28 ONEN
[1] Kama theluji wakati wa kiangazi au mvua wakati wa mavuno, ndivyo asivyostahili heshima mpumbavu. [2] Kama shomoro apigapigavyo mabawa yake au mbayuwayu katika kuruka kwake kasi, ndivyo ilivyo laana isiyo na sababu haimpati mtu. [3] Mjeledi kwa farasi, lijamu kwa punda, nayo fimbo kwa migongo ya wapumbavu! [4] Usimjibu mpumbavu sawasawa na upumbavu wake, ama wewe mwenyewe utakuwa kama yeye. [5] Mjibu mpumbavu sawasawa na upumbavu wake, ama atakuwa mwenye hekima machoni pake mwenyewe. [6] Kama vile ilivyo kujikata miguu au kunywa hasara, ndivyo ilivyo kutuma ujumbe kwa mkono wa mpumbavu. [7] Kama miguu ya kiwete inavyoningʼinia ndivyo ilivyo mithali katika kinywa cha mpumbavu. [8] Kama kufunga jiwe kwenye kombeo, ndivyo ilivyo kumpa mpumbavu heshima. [9] Kama mwiba kwenye mkono wa mlevi ndivyo ilivyo mithali kinywani mwa mpumbavu. [10] Kama mpiga upinde ambaye hujeruhi ovyo, ndivyo alivyo yeye aajiriye mpumbavu au yeyote apitaye njiani. [11] Kama mbwa ayarudiavyo matapiko yake, ndivyo mpumbavu arudiavyo upumbavu wake. [12] Je, unamwona mtu ajionaye mwenye hekima machoni pake mwenyewe? Liko tumaini zaidi kwa mpumbavu kuliko kwake. [13] Mvivu husema, “Yuko simba barabarani, simba mkali anazunguka mitaa!” [14] Kama vile mlango ugeukavyo kwenye bawaba zake, ndivyo mvivu ajigeuzavyo kitandani mwake. [15] Mtu mvivu hutumbukiza mkono wake kwenye sahani, naye huchoka kuupeleka kwenye kinywa chake. [16] Mtu mvivu ni mwenye hekima machoni pake mwenyewe, kuliko watu saba wawezao kujibu kwa busara. [17] Kama yeye amkamataye mbwa kwa masikio, ndivyo alivyo mtu apitaye njiani na kujiingiza kwenye ugomvi usiomhusu. [18] Kama mtu mwendawazimu atupaye vijinga vya moto au mishale ya kufisha, [19] ndivyo alivyo mtu amdanganyaye jirani yake na kusema, “Nilikuwa nikifanya mzaha tu!” [20] Bila kuni moto huzimika; pasipo uchongezi ugomvi humalizika. [21] Kama makaa juu ya makaa yanayowaka, na kama kuni kwenye moto, ndivyo alivyo mtu mgomvi kwa kuchochea ugomvi. [22] Maneno ya mchongezi ni kama chakula kitamu; huingia sehemu za ndani sana za mtu. [23] Kama rangi ingʼaayo iliyopakwa kwenye vyombo vya udongo ndivyo ilivyo midomo laini pamoja na moyo mbaya. [24] Mtu mwenye nia ya kudhuru wengine hujificha kwa maneno ya midomo yake, lakini moyoni mwake huficha udanganyifu. [25] Ingawa maneno yake huvutia, usimwamini, kwa maana machukizo saba hujaza moyo wake. [26] Nia yake ya kudhuru wengine inaweza kufichwa na udanganyifu, lakini uovu wake utafichuliwa kwenye kusanyiko. [27] Kama mtu akichimba shimo, atatumbukia ndani yake, kama mtu akivingirisha jiwe, litamrudia. [28] Ulimi wa uongo, huwachukia wale unaowaumiza, nacho kinywa cha kujipendekeza hutenda uharibifu.
