Mithali 23:1-35 ONEN
[1] Uketipo kula chakula na mtawala, angalia vyema kile kilicho mbele yako, [2] na utie kisu kooni mwako kama ukiwa mlafi. [3] Usitamani vyakula vyake vitamu kwa kuwa chakula hicho ni cha hila. [4] Usijitaabishe ili kuupata utajiri, uwe na hekima kuonyesha kujizuia. [5] Kufumba na kufumbua utajiri hutoweka, huwa kama umepata mabawa ghafula, ukaruka na kutoweka angani kama tai. [6] Usile chakula cha mtu mchoyo, usitamani vyakula vyake vitamu, [7] kwa maana yeye ni aina ya mtu ambaye kila mara anafikiri juu ya gharama. Anakuambia, “Kula na kunywa,” lakini moyo wake hauko pamoja nawe. [8] Utatapika kile kidogo ulichokula, nawe utakuwa umepoteza bure maneno yako ya kumsifu. [9] Usizungumze na mpumbavu, kwa maana atadhihaki hekima ya maneno yako. [10] Usisogeze jiwe la mpaka wa zamani wala kunyemelea kwenye mashamba ya yatima, [11] kwa kuwa Mtetezi wao ni mwenye nguvu, atalichukua shauri lao dhidi yako. [12] Elekeza moyo wako kwenye mafundisho na masikio yako kwenye maneno ya maarifa. [13] Usimnyime mtoto adhabu, ukimwadhibu kwa fimbo, hatakufa. [14] Mwadhibu kwa fimbo na kuiokoa nafsi yake kutoka mautini. [15] Mwanangu, kama moyo wako una hekima, basi moyo wangu utafurahi, [16] utu wangu wa ndani utafurahi, wakati midomo yako itakapozungumza lililo sawa. [17] Usiuruhusu moyo wako kuwaonea wivu wenye dhambi, bali kila mara uwe na bidii katika kumcha BWANA. [18] Hakika kuna tumaini la baadaye kwa ajili yako, nalo tarajio lako halitakatiliwa mbali. [19] Sikiliza, mwanangu na uwe na hekima, weka moyo wako kwenye njia iliyo sawa. [20] Usiwe miongoni mwa wanywao mvinyo, au wale walao nyama kwa pupa, [21] kwa maana walevi na walafi huwa maskini, nako kusinzia huwavika matambara. [22] Msikilize baba yako, aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako atakapokuwa mzee. [23] Nunua kweli wala usiiuze, pata hekima, adabu na ufahamu. [24] Baba wa mwenye haki ana furaha kubwa, naye aliye na mwana mwenye hekima humfurahia. [25] Baba yako na mama yako na wafurahi, mama aliyekuzaa na ashangilie! [26] Mwanangu, nipe moyo wako, macho yako na yafuate njia zangu, [27] kwa maana kahaba ni shimo refu na mwanamke mpotovu ni kisima chembamba. [28] Kama mnyangʼanyi, hungojea akivizia, naye huzidisha wasio waaminifu miongoni mwa wanaume. [29] Ni nani mwenye ole? Ni nani mwenye huzuni? Ni nani mwenye ugomvi? Ni nani mwenye malalamiko? Ni nani aliye na majeraha yasiyo na sababu? Ni nani mwenye macho mekundu? [30] Ni hao wakaao sana kwenye mvinyo, hao waendao kuonja mabakuli ya mvinyo uliochanganywa. [31] Usiukodolee macho mvinyo wakati ukiwa mwekundu, wakati unapometameta kwenye bilauri, wakati ushukapo taratibu! [32] Mwishowe huuma kama nyoka na kutia sumu yake kama nyoka mwenye sumu. [33] Macho yako yataona mambo mageni na moyo wako kuwazia mambo yaliyopotoka. [34] Utakuwa kama alalaye katikati ya bahari, alalaye juu ya kamba ya merikebu. [35] Utasema, “Wamenipiga lakini sikuumia! Wamenichapa, lakini sisikii! Nitaamka lini ili nikanywe tena?”
