Mithali 24:1-34 ONEN
[1] Usiwaonee wivu watu waovu, usitamani ushirika nao; [2] kwa maana mioyo yao hupanga mambo ya jeuri, nayo midomo yao husema juu ya kuleta madhara. [3] Kwa hekima nyumba hujengwa, nayo kwa njia ya ufahamu huimarishwa [4] kwa njia ya maarifa vyumba vyake hujazwa vitu vya thamani na vya kupendeza. [5] Mtu mwenye hekima ana uwezo mkubwa, naye mtu mwenye maarifa huongeza nguvu, [6] kwa kufanya vita unahitaji uongozi na kwa ushindi washauri wengi. [7] Hekima i juu mno kwa mpumbavu, katika kusanyiko langoni hana lolote la kusema. [8] Yeye apangaye mabaya atajulikana kama mtu wa hila. [9] Mipango ya upumbavu ni dhambi, watu huchukizwa na mwenye dhihaka. [10] Ukikata tamaa wakati wa taabu, jinsi gani nguvu zako ni kidogo! [11] Okoa wale wanaoongozwa kwenye kifo; wazuie wote wanaojikokota kuelekea machinjoni. [12] Kama mkisema, “Lakini hatukujua lolote kuhusu hili,” je, yule apimaye mioyo halitambui hili? Je, yule awalindaye maisha yenu halijui hili? Je, hatamlipa kila mtu kulingana na aliyotenda? [13] Ule asali mwanangu, kwa kuwa ni nzuri; asali kutoka kwenye sega ni tamu kwa kuonja. [14] Ujue pia kwamba hekima ni tamu kwa nafsi yako, kama ukiipata, kuna matumaini kwako ya siku zijazo, nalo tumaini lako halitakatiliwa mbali. [15] Usivizie kama haramia afanyavyo ili kuyashambulia makao ya mwenye haki, wala usiyavamie makazi yake, [16] Kwa maana ingawa mtu mwenye haki huanguka mara saba, huinuka tena, lakini waovu huangushwa chini na maafa. [17] Usitazame kwa kufurahia adui yako aangukapo; wakati ajikwaapo, usiruhusu moyo wako ushangilie. [18] BWANA asije akaona na kuchukia akaiondoa ghadhabu yake mbali naye. [19] Usikasirike kwa sababu ya watu wabaya wala usiwaonee wivu waovu, [20] kwa maana mtu mbaya hana tumaini la siku zijazo, nayo taa ya waovu itazimwa. [21] Mwanangu, mche BWANA na mfalme, wala usijiunge na waasi, [22] kwa maana hao wawili watatuma maangamizi ya ghafula juu yao, naye ni nani ajuaye maafa wawezayo kuleta? [23] Hii pia ni misemo ya wenye hekima: Kuonyesha upendeleo katika hukumu si vyema: [24] Yeyote amwambiaye mwenye hatia, “Wewe huna hatia,” Kabila zitamlaani na mataifa yatamkana. [25] Bali itakuwa vyema kwa wale watakaowatia hatiani wenye hatia, nazo baraka tele zitawajilia juu yao. [26] Jawabu la uaminifu ni kama busu la midomoni. [27] Maliza kazi zako za nje, nawe uweke mashamba yako tayari, baada ya hayo, jenga nyumba yako. [28] Usishuhudie dhidi ya jirani yako bila sababu, au kutumia midomo yako kudanganya. [29] Usiseme, “Nitamtenda kama alivyonitenda mimi; nitamlipiza mtu yule kwa kile alichonitendea.” [30] Nilipita karibu na shamba la mvivu, karibu na shamba la mizabibu la mtu asiye na akili, [31] miiba ilikuwa imeota kila mahali, ardhi ilikuwa imefunikwa na magugu, na ukuta wa mawe ulikuwa umebomoka. [32] Nikatafakari moyoni mwangu lile nililoliona, nami nikajifunza somo kutokana na niliyoyaona: [33] Bado kulala kidogo, kusinzia kidogo, bado kukunja mikono kidogo upate kupumzika: [34] hivyo umaskini utakuja juu yako kama mnyangʼanyi, na kupungukiwa kutakujia kama mtu mwenye silaha.
