Mithali 22:1-29 ONEN
[1] Heri kuchagua jina jema kuliko utajiri mwingi, kuheshimiwa ni bora kuliko fedha au dhahabu. [2] Tajiri na maskini wanafanana kwa hili: BWANA ni Muumba wao wote. [3] Mtu mwenye busara huona hatari na kujificha, bali mjinga huendelea mbele kama kipofu nayo ikamtesa. [4] Unyenyekevu na kumcha BWANA huleta utajiri, heshima na uzima. [5] Katika mapito ya waovu kuna miiba na mitego, bali yeye ailindaye nafsi yake hukaa mbali nayo. [6] Mfundishe mtoto njia impasayo kuiendea, naye hataiacha hata akiwa mzee. [7] Matajiri huwatawala maskini naye akopaye ni mtumwa wa akopeshaye. [8] Yeye aupandaye uovu huvuna taabu, nayo fimbo ya ghadhabu yake itaangamizwa. [9] Mtu mkarimu yeye mwenyewe atabarikiwa kwa kuwa hushiriki chakula chake na maskini. [10] Mfukuze mwenye dhihaka, na mvutano utatoweka; ugomvi na matukano vitakoma. [11] Yeye apendaye moyo safi na yeye ambaye maneno yake ni ya neema, mfalme atakuwa rafiki yake. [12] Macho ya BWANA hulinda maarifa, bali huyapinga maneno ya asiye mwaminifu. [13] Mvivu husema, “Yuko simba nje!” au, “Nitauawa katika mitaa!” [14] Kinywa cha mwanamke kahaba ni shimo refu; yeye aliye chini ya ghadhabu ya BWANA atatumbukia ndani yake. [15] Upumbavu umefungwa ndani ya moyo wa mtoto, bali fimbo ya adhabu itaufukuzia mbali naye. [16] Yeye amwoneaye maskini ili kujiongezea mali, naye ampaye tajiri zawadi, wote huwa maskini. [17] Tega sikio na usikie misemo ya wenye hekima, elekeza moyo wako kwenye yale nifundishayo, [18] kwa maana inapendeza unapoyahifadhi moyoni mwako na kuwa nayo yote tayari midomoni mwako. [19] Ili tumaini lako liwe katika BWANA, hata wewe, ninakufundisha leo. [20] Je, sijakuandikia misemo thelathini, misemo ya mashauri na maarifa, [21] kukufundisha maneno ya kweli na ya kuaminika, ili uweze kutoa majibu sahihi kwake yeye aliyekutuma? [22] Usiwadhulumu maskini kwa sababu ni maskini, wala kumdhulumu mhitaji mahakamani, [23] kwa sababu BWANA atalichukua shauri lao naye atawateka wao waliowateka. [24] Usifanye urafiki na mtu mwenye hasira ya haraka, usishirikiane na yule aliye mwepesi kukasirika, [25] la sivyo utajifunza njia zake na kujiingiza mwenyewe kwenye mtego. [26] Usiwe mwenye kupana mikono katika rehani, au kuweka dhamana kwa ajili ya madeni. [27] Kama ukikosa njia ya kulipa, kitanda chako kitachukuliwa ukiwa umekilalia. [28] Usisogeze jiwe la mpaka wa zamani lililowekwa na baba zako. [29] Je, unamwona mtu stadi katika kazi yake? Atahudumu mbele ya wafalme; hatahudumu mbele ya watu duni.
