Mithali 21:1-31 ONEN
[1] Moyo wa mfalme uko katika mkono wa BWANA; huuongoza kama mkondo wa maji, popote apendapo. [2] Njia zote za mwanadamu huonekana sawa kwake, bali BWANA huupima moyo. [3] Kufanya yaliyo sawa na haki inakubalika zaidi kwa BWANA kuliko dhabihu. [4] Macho ya kudharau na moyo wa kiburi, ambavyo ni taa ya waovu, vyote ni dhambi! [5] Mipango ya mwenye bidii huelekeza kwenye faida, kama vile kwa hakika pupa huelekeza kwenye umaskini. [6] Mali iliyopatikana kwa ulimi wa uongo ni mvuke upitao upesi na mtego wa kufisha. [7] Jeuri ya waovu itawaburuta mbali, kwa kuwa wanakataa kufanya yaliyo sawa. [8] Njia ya mwenye hatia ni ya upotovu, bali tabia ya mtu asiye na hatia ni nyofu. [9] Ni afadhali kuishi pembeni mwa paa la nyumba, kuliko kuishi nyumba moja na mke mgomvi. [10] Mtu mwovu hutamani sana ubaya, jirani yake hapati huruma kutoka kwake. [11] Wakati mwenye mzaha ameadhibiwa, mjinga hupata hekima; wakati mtu mwenye hekima afundishwapo, hupata maarifa. [12] Mwenye Haki huyajua yanayotendeka katika nyumba za waovu, naye atawaangamiza waovu. [13] Mtu akiziba masikio asisikie kilio cha maskini, yeye pia atalia, wala hatajibiwa. [14] Zawadi itolewayo kwa siri hutuliza hasira na rushwa iliyofichwa kwenye nguo hutuliza ghadhabu kali. [15] Wakati haki imetendeka, huleta furaha kwa wenye haki, bali kitisho kwa watenda mabaya. [16] Mtu anayepotea kutoka mapito ya ufahamu, hupumzika katika kundi la waliokufa. [17] Mtu apendaye anasa atakuwa maskini, yeyote apendaye mvinyo na mafuta kamwe hatakuwa tajiri. [18] Waovu huwa fidia kwa ajili ya wenye haki, nao wasio waaminifu kwa ajili ya wanyofu. [19] Ni afadhali kuishi jangwani kuliko kuishi na mke mgomvi na mkorofi. [20] Katika nyumba ya mwenye hekima kuna akiba ya vyakula vizuri na mafuta, lakini mtu mpumbavu hutafuna vyote alivyo navyo. [21] Yeye afuatiaye haki na upendo hupata uzima, mafanikio na heshima. [22] Mtu mwenye hekima huushambulia mji wa wenye nguvu, na kuangusha ngome wanazozitegemea. [23] Yeye alindaye kinywa chake na ulimi wake hujilinda na maafa. [24] Mtu mwenye kiburi na majivuno, “Mdhihaki” ndilo jina lake; hutenda mambo kwa kiburi kilichozidi. [25] Kutamani sana kwa mvivu kutakuwa kifo chake, kwa sababu mikono yake haitaki kufanya kazi. [26] Mchana kutwa hutamani zaidi, lakini mnyofu hutoa pasipo kuzuia. [27] Dhabihu ya mtu mwovu ni chukizo, si zaidi sana itolewapo kwa nia mbaya! [28] Shahidi wa uongo ataangamia, bali maneno ya mwenye kusikia yatadumu. [29] Mtu mwovu ana uso wa ushupavu, bali mtu mnyofu huzifikiria njia zake. [30] Hakuna hekima, wala akili, wala mpango unaoweza kufaulu dhidi ya BWANA. [31] Farasi huandaliwa kwa ajili ya siku ya vita, bali ushindi huwa kwa BWANA.
