Mithali 20:1-30 ONEN
[1] Mvinyo ni mdhihaki na kileo ni mgomvi; yeyote apotoshwaye navyo hana hekima. [2] Ghadhabu ya mfalme ni kama ngurumo ya simba; yeye amkasirishaye hupoteza uhai wake. [3] Ni kwa heshima ya mtu kujitenga ugomvi, bali kila mpumbavu ni mwepesi kugombana. [4] Mvivu halimi kwa majira; kwa hiyo wakati wa mavuno hutazama lakini hapati chochote. [5] Makusudi ya moyo wa mwanadamu ni maji yenye kina, lakini mtu mwenye ufahamu huyachota. [6] Watu wengi hujidai kuwa na upendo usiokoma, bali mtu mwaminifu ni nani awezaye kumpata? [7] Mtu mwenye haki huishi maisha yasiyo na lawama, wamebarikiwa watoto wake baada yake. [8] Wakati mfalme aketipo katika kiti chake cha enzi kuhukumu, hupepeta ubaya wote kwa macho yake. [9] Ni nani awezaye kusema, “Nimeuweka moyo wangu safi; mimi ni safi na sina dhambi?” [10] Mawe ya kupimia yaliyo tofauti na vipimo tofauti, BWANA huchukia vyote viwili. [11] Hata mtoto hujulikana kwa matendo yake, kama tabia yake ni safi na adili. [12] Masikio yasikiayo na macho yaonayo, BWANA ndiye alivifanya vyote viwili. [13] Usiupende usingizi la sivyo utakuwa maskini, uwe macho nawe utakuwa na chakula cha akiba. [14] “Haifai, haifai!” asema mnunuzi, kisha huondoka akijisifia ununuzi wake. [15] Dhahabu kunayo, na marijani kwa wingi, lakini midomo inenayo maarifa ni kito cha thamani kilicho adimu. [16] Chukua vazi la yule awekaye dhamana kwa ajili ya mgeni; lishikilie iwe dhamana kama anafanya hivyo kwa ajili ya mwanamke mpotovu. [17] Chakula kilichopatikana kwa hila ni kitamu kwa mwanadamu, bali huishia na kinywa kilichojaa changarawe. [18] Fanya mipango kwa kutafuta mashauri, ukipigana vita, tafuta maelekezo. [19] Maneno ya kusengenya husababisha kutokuaminika, kwa hiyo mwepuke mtu anayezungumza kupita kiasi. [20] Ikiwa mtu atamlaani baba yake au mama yake, taa yake itazimwa katika giza nene. [21] Urithi upatikanao haraka mwanzoni, hautabarikiwa mwishoni. [22] Usiseme, “Nitakulipiza kwa ajili ya kosa hili!” Mngojee BWANA, naye atakuokoa. [23] BWANA anachukia sana mawe ya kupimia ya udanganyifu, nazo mizani zisizo halali hazimpendezi. [24] Hatua za mtu huongozwa na BWANA. Anawezaje basi mtu yeyote kuelewa njia yake mwenyewe? [25] Ni mtego kwa mtu kuweka wakfu kitu kwa haraka na baada ya kitambo kidogo kufikiria tena nadhiri zake. [26] Mfalme mwenye hekima hupepeta waovu, hulipitisha gurudumu la kupuria juu yao. [27] Taa ya BWANA huchunguza roho ya mwanadamu, huchunguza utu wake wa ndani. [28] Upendo na uaminifu humweka mfalme salama, kwa njia ya upendo, kiti chake cha enzi huwa salama. [29] Utukufu wa vijana ni nguvu zao, mvi ni fahari ya uzee. [30] Mapigo na majeraha huusafisha ubaya, nayo michapo hutakasa utu wa ndani.
