Mithali 19:1-29 ONEN
[1] Afadhali mtu maskini ambaye mwenendo wake hauna lawama, kuliko mpumbavu ambaye midomo yake imepotoka. [2] Sio vizuri kuwa na juhudi bila maarifa, wala kufanya haraka na kuikosa njia. [3] Upumbavu wa mtu mwenyewe huharibu maisha yake hata hivyo moyo wake humkasirikia BWANA. [4] Mali huleta marafiki wengi, bali rafiki wa mtu maskini humwacha. [5] Shahidi wa uongo hataacha kuadhibiwa, naye amwagaye uongo hataachwa huru. [6] Wengi hujipendekeza kwa mtawala na kila mmoja ni rafiki wa mtu atoaye zawadi. [7] Mtu maskini huepukwa na ndugu zake wote: Je, marafiki zake watamkwepa kiasi gani! Ingawa huwafuata kwa kuwasihi, hawapatikani popote. [8] Yeye apataye hekima huipenda nafsi yake mwenyewe, yeye ahifadhiye ufahamu hustawi. [9] Shahidi wa uongo hataacha kuadhibiwa, naye amwagaye uongo ataangamia. [10] Haistahili mpumbavu kuishi katika anasa, itakuwa vibaya kiasi gani kwa mtumwa kuwatawala wakuu. [11] Hekima ya mtu humpa uvumilivu, ni kwa utukufu wake kusamehe makosa. [12] Ghadhabu ya mfalme ni kama mngurumo wa simba, bali wema wake ni kama umande juu ya nyasi. [13] Mwana mpumbavu ni maangamizi ya babaye, naye mke mgomvi ni kama kutonatona kusikoisha. [14] Nyumba na mali hurithiwa kutoka kwa wazazi, bali mke mwenye busara hutoka kwa BWANA. [15] Uvivu huleta usingizi mzito, naye mtu mzembe huona njaa. [16] Yeye ambaye hutii mafundisho huulinda uhai wake, bali yeye anayezidharau njia zake atakufa. [17] Yeye amhurumiaye maskini humkopesha BWANA, naye atamtuza kwa aliyotenda. [18] Mrudi mwanao, kwa maana katika hiyo kuna tumaini, usiwe mshirika katika mauti yake. [19] Mtu mwenye kukasirika haraka ni lazima atapata adhabu yake, kama utamwokoa, itakubidi kufanya hivyo tena. [20] Sikiliza mashauri na ukubali mafundisho, nawe mwishoni utakuwa na hekima. [21] Kuna mipango mingi ndani ya moyo wa mtu, lakini kusudi la BWANA ndilo litakalosimama. [22] Lile mtu alionealo shauku ni upendo usio na mwisho, afadhali kuwa maskini kuliko kuwa mwongo. [23] Kumcha BWANA huongoza kwenye uzima, kisha mtu hupumzika akiwa ameridhika, bila kuguswa na shida. [24] Mtu mvivu hutumbukiza mkono wake kwenye sahani, lakini hawezi hata kuupeleka kwenye kinywa chake! [25] Mpige mwenye mzaha, naye mjinga atajifunza busara, mkemee mwenye ufahamu naye atapata maarifa. [26] Yeye amwibiaye baba yake na kumfukuza mama yake ni mwana aletaye aibu na fedheha. [27] Mwanangu, ukiacha kusikiliza mafundisho, utatangatanga mbali na maneno ya maarifa. [28] Shahidi mla rushwa hudhihaki hukumu na kinywa cha mtu mwovu humeza ubaya kwa upesi. [29] Adhabu zimeandaliwa kwa ajili ya wenye dhihaka na mapigo kwa ajili ya migongo ya wapumbavu.
