Mithali 1:1-33 ONEN
[1] Mithali za Solomoni mwana wa Daudi, mfalme wa Israeli: [2] Kwa kupata hekima na nidhamu; kwa kufahamu maneno ya busara; [3] kwa kujipatia nidhamu na busara, kufanya lililo sawa, haki na bila kupendelea; [4] huwapa busara wajinga, maarifa na akili kwa vijana; [5] wenye hekima na wasikilize nao waongeze elimu yao, wenye kupambanua na wapate mwongozo; [6] kwa kufahamu mithali na mifano, misemo na vitendawili vya wenye hekima. [7] Kumcha BWANA ndicho chanzo cha maarifa, lakini wapumbavu hudharau hekima na adabu. [8] Mwanangu, sikiliza mwongozo wa baba yako, wala usiyaache mafundisho ya mama yako. [9] Hayo yatakuwa taji la maua la neema kichwani pako, na mkufu wa kuipamba shingo yako. [10] Mwanangu, kama wenye dhambi wakikushawishi, usikubaliane nao. [11] Kama wakisema, “Twende tufuatane; tukamvizie mtu na kumwaga damu, njoo tukavizie nafsi isiyo na hatia; [12] tuwameze wakiwa hai kama kaburi, wakiwa wazima kama wale wanaotumbukia shimoni. [13] Tutapata aina zote za vitu vya thamani na kujaza nyumba zetu kwa nyara. [14] Njoo ushirikiane nasi, vitu vyote tutakavyopata tutagawana.” [15] Mwanangu, usiandamane nao. Usiweke mguu wako katika njia zao, [16] kwa kuwa miguu yao hukimbilia kwenye dhambi, ni wepesi kumwaga damu. [17] Tazama ni jinsi gani ilivyo kazi bure kutandaza wavu wakati ndege wote wanakuona! [18] Watu hawa huvizia kumwaga damu yao wenyewe; hujivizia tu wenyewe! [19] Huu ndio mwisho wa wote ambao wanajipatia mali kwa hila; huuondoa uhai wa wale wenye mali. [20] Hekima huita kwa sauti kuu barabarani, hupaza sauti yake kwenye viwanja vikubwa; [21] kwenye makutano ya barabara za mji zenye makelele mengi hupaza sauti, kwenye malango ya mji hutoa hotuba yake: [22] “Enyi wajinga, mtangʼangʼania ujinga wenu hadi lini? Mpaka lini wenye mizaha watafurahia mizaha, na wapumbavu kuchukia maarifa? [23] Kama mngekuwa mmeitikia karipio langu, ningekuwa nimemimina roho yangu kwenu na kuwafahamisha maneno yangu. [24] Lakini kwa kuwa mlinikataa nilipowaita na hakuna yeyote aliyekubali niliponyoosha mkono wangu, [25] kwa kuwa mliyapuuza mashauri yangu yote na hamkukubali karipio langu, [26] mimi nami nitawacheka katika maafa yenu, nitawadhihaki wakati janga litawapata: [27] wakati janga litawapata kama tufani, wakati maafa yatawazoa kama upepo wa kisulisuli, wakati dhiki na taabu zitawalemea. [28] “Ndipo watakaponiita lakini sitawajibu; watanitafuta lakini hawatanipata. [29] Kwa kuwa walichukia maarifa, wala hawakuchagua kumcha BWANA, [30] kwa kuwa hawakukubali mashauri yangu, na kukataa maonyo yangu, [31] watakula matunda ya njia zao, na watashibishwa matunda ya hila zao. [32] Kwa kuwa ukaidi wa wajinga utawaua, nako kuridhika kwa wajinga kutawaangamiza. [33] Lakini yeyote anisikilizaye ataishi kwa usalama, atatulia, bila kuwa na hofu ya madhara.”
