[1] Mtu ajitengaye na wengine hufuata matakwa yake mwenyewe; hupiga vita kila shauri jema. [2] Mpumbavu hafurahii ufahamu, bali hufurahia kutangaza maoni yake mwenyewe. [3] Wakati uovu unapokuja, dharau huja pia, pamoja na aibu huja lawama. [4] Maneno ya kinywa cha mwanadamu ni kina cha maji, bali chemchemi ya hekima ni kijito kinachobubujika. [5] Sio vizuri kumpendelea mtu mwovu, au kumnyima haki asiye na hatia. [6] Midomo ya mpumbavu humletea ugomvi na kinywa chake hualika kipigo. [7] Kinywa cha mpumbavu ni uharibifu wake na midomo yake ni mtego kwa nafsi yake. [8] Maneno ya mchongezi ni kama chakula kitamu; huingia sehemu za ndani sana za mtu. [9] Mtu aliye mlegevu katika kazi yake ni ndugu na yule anayeharibu. [10] Jina la BWANA ni ngome imara, wenye haki huikimbilia na kuwa salama. [11] Mali ya tajiri ni mji wake wenye ngome, wanaudhania kuwa ukuta usioweza kurukwa. [12] Kabla ya anguko moyo wa mtu hujaa kiburi, bali unyenyekevu hutangulia heshima. [13] Yeye ajibuye kabla ya kusikiliza, huo ni upumbavu wake na aibu yake. [14] Roho ya mtu itastahimili katika ugonjwa bali roho iliyovunjika ni nani awezaye kuistahimili? [15] Moyo wa mwenye ufahamu hujipatia maarifa, masikio ya mwenye hekima huyatafuta maarifa. [16] Zawadi humfungulia njia mtoaji, nayo humleta mbele ya wakuu. [17] Yeye aliye wa kwanza kuleta mashtaka huonekana sahihi, hadi mwingine ajitokezapo na kumuuliza maswali. [18] Kupiga kura hukomesha mashindano na kutenganisha wapinzani wakuu wanaopingana. [19] Ndugu aliyechukizwa ni mgumu kuridhika kuliko mji uliozungushiwa ngome, nayo mabishano ni kama malango ya ngome yenye makomeo. [20] Tumbo la mtu litajaa kutokana na tunda la kinywa chake, atashibishwa mavuno yanayotokana na midomo yake. [21] Mauti na uzima viko katika uwezo wa ulimi, nao waupendao watakula matunda yake. [22] Apataye mke apata kitu chema naye ajipatia kibali kwa BWANA. [23] Mtu maskini huomba kuhurumiwa bali tajiri hujibu kwa ukali. [24] Mtu mwenye marafiki wengi wanaweza kumharibu, bali yuko rafiki aambatanaye na mtu kwa karibu kuliko ndugu.