Mithali 17:1-28 ONEN
[1] Afadhali kula ukoko mkavu ukiwa na amani na utulivu kuliko kukaa kwenye nyumba ya karamu kukiwa na magomvi. [2] Mtumishi mwenye hekima atatawala juu ya mwana aaibishaye, naye atashirikiana katika urithi kama mmoja wa hao ndugu. [3] Kalibu ni kwa ajili ya fedha na tanuru ni kwa ajili ya dhahabu, bali BWANA huujaribu moyo. [4] Mtu mwovu husikiliza midomo mibaya; mwongo husikiliza kwa makini ulimi wa madhara. [5] Yeye anaye mdhihaki maskini huonyesha dharau kwa Muumba wake; yeyote afurahiaye maafa hataepuka kuadhibiwa. [6] Wana wa wana ni taji la wazee, nao wazazi ni fahari ya watoto wao. [7] Midomo yenye uwezo wa ushawishi haimfai mpumbavu: je, ni mibaya kiasi gani zaidi midomo ya uongo kwa mtawala! [8] Kipawa ni kama kito cha thamani machoni pake yeye aliye nacho; kokote kigeukiapo, hufanikiwa. [9] Yeye anayesamehe kosa hudumisha upendo, bali yeyote arudiaye jambo hutenganisha marafiki wa karibu. [10] Karipio humwingia sana mtu mwenye kutambua kuliko mapigo mia kwa mpumbavu. [11] Mtu mbaya hupenda kuasi tu; mjumbe asiye na huruma atatumwa dhidi yake. [12] Ni afadhali ukutane na dubu aliyenyangʼanywa watoto wake, kuliko mpumbavu katika upumbavu wake. [13] Ikiwa mtu atalipa baya kwa jema, kamwe ubaya hautaondoka katika nyumba yake. [14] Kuanzisha ugomvi ni kama kutoboa bwawa la maji; kwa hiyo acha jambo hilo kabla mabishano hayajaanza. [15] Yeye asemaye kuwa asiye na haki ana haki, naye asemaye kuwa mwenye haki hana haki: BWANA huwachukia sana wote wawili. [16] Fedha ina faida gani mikononi mwa mpumbavu, wakati yeye hana haja ya kupata hekima? [17] Rafiki hupenda wakati wote naye ndugu amezaliwa kwa ajili ya wakati wa shida. [18] Mtu mjinga hupana mkono ili kuweka rehani, naye huweka dhamana kwa jirani yake. [19] Yeye apendaye ugomvi apenda dhambi; naye ainuaye sana lango lake hutafuta uharibifu. [20] Mtu mwenye moyo mpotovu hawezi kufanikiwa; naye ambaye ulimi wake ni mdanganyifu huanguka kwenye taabu. [21] Kuwa na mwana mpumbavu huleta huzuni; hakuna furaha kwa baba wa mpumbavu. [22] Moyo wenye furaha ni dawa nzuri, bali roho iliyopondeka hukausha mifupa. [23] Mtu mwovu hukubali rushwa kwa siri ili kupotosha njia ya haki. [24] Mtu wa ufahamu huitazama hekima, lakini macho ya mpumbavu huhangaika hadi kwenye miisho ya dunia. [25] Mwana mpumbavu huleta huzuni kwa baba yake na uchungu kwa yeye aliyemzaa. [26] Si vizuri kumwadhibu mtu asiye na hatia, au kuwapiga sana maafisa kwa ajili ya uadilifu wao. [27] Mtu mwenye maarifa hutumia maneno kwa kujizuia, naye mtu mwenye ufahamu ana moyo wa utulivu. [28] Hata mtu mpumbavu hudhaniwa kuwa na hekima kama akinyamaza, na mwenye ufahamu kama akiuzuia ulimi wake.
