Mithali 16:1-33 ONEN
[1] Mipango ya moyoni ni ya mwanadamu, bali jibu la ulimi hutoka kwa BWANA. [2] Njia zote za mtu huonekana safi machoni pake mwenyewe, bali makusudi hupimwa na BWANA. [3] Mkabidhi BWANA lolote ufanyalo, nayo mipango yako itafanikiwa. [4] BWANA hufanya kila kitu kwa kusudi lake mwenyewe; hata waovu kwa siku ya maangamizi. [5] BWANA huwachukia sana wote wenye kiburi cha moyo. Uwe na hakika kwa hili: Hawataepuka kuadhibiwa. [6] Kwa upendo na uaminifu uovu huondolewa; kwa kumcha BWANA mtu hujiepusha na ubaya. [7] Njia za mtu zinapompendeza BWANA, huwafanya hata adui zake waishi naye kwa amani. [8] Afadhali kitu kidogo pamoja na haki kuliko mapato mengi pamoja na udhalimu. [9] Moyo wa mtu huifikiri njia yake, bali BWANA huelekeza hatua zake. [10] Midomo ya mfalme huzungumza kwa hekima ya kiungu, wala kinywa chake hakipotoshi haki. [11] Vipimo na mizani za halali hutoka kwa BWANA; mawe yote ya kupimia yaliyo katika mfuko ameyafanya yeye. [12] Wafalme huchukia sana kutenda maovu, kwa maana kiti cha ufalme hufanywa imara kwa njia ya haki. [13] Wafalme hufurahia midomo ya uaminifu; humthamini mtu asemaye kweli. [14] Ghadhabu ya mfalme ni mjumbe wa mauti, bali mtu mwenye hekima ataituliza. [15] Uso wa mfalme ungʼaapo, inamaanisha uhai; upendeleo wake ni kama wingu la mvua wakati wa vuli. [16] Ni bora kiasi gani kupata hekima kuliko dhahabu, kuchagua ufahamu kuliko fedha! [17] Njia kuu ya wanyofu huepuka ubaya; yeye aichungaye njia yake, huchunga maisha yake. [18] Kiburi hutangulia maangamizi, roho ya majivuno hutangulia maanguko. [19] Ni afadhali kuwa mnyenyekevu katika roho miongoni mwa walioonewa kuliko kugawana nyara pamoja na wenye kiburi. [20] Yeyote anayekubali mafundisho hustawi, tena amebarikiwa yeye anayemtumaini BWANA. [21] Wenye hekima moyoni huitwa wenye ufahamu, na maneno ya kupendeza huchochea mafundisho. [22] Ufahamu ni chemchemi ya uzima kwa wale walio nao, bali upumbavu huleta adhabu kwa wapumbavu. [23] Moyo wa mtu mwenye hekima huongoza kinywa chake, na midomo yake huchochea mafundisho. [24] Maneno ya kupendeza ni kama sega la asali, ni matamu kwa nafsi na uponyaji kwenye mifupa. [25] Iko njia ionekanayo kuwa sawa kwa mtu, bali mwisho wake huelekeza mautini. [26] Shauku ya mfanyakazi humhimiza kufanya kazi; njaa yake humsukuma aendelee. [27] Mtu mbaya kabisa hupanga mabaya, maneno yake ni kama moto uunguzao. [28] Mtu mpotovu huchochea ugomvi, nayo maongezi ya upuzi hutenganisha marafiki wa karibu. [29] Mtu mkali humvuta jirani yake na kumwongoza katika mapito yale mabaya. [30] Yeye akonyezaye kwa jicho lake anapanga upotovu; naye akazaye midomo yake amenuia mabaya. [31] Mvi ni taji ya utukufu; hupatikana kwa maisha ya uadilifu. [32] Ni afadhali mtu mstahimilivu kuliko shujaa, mtu anayeitawala hasira yake kuliko yule autekaye mji. [33] Kura hupigwa kwa siri, lakini kila uamuzi wake hutoka kwa BWANA.
